Zoezi la kuhakiki vyeti na kuandikisha vitambulisho vya kitaifa Wilaya ya Kishatu mkoani Shinyanga limeingia dosari baada ya vifaa vinavyotumika kuendeshea zoezi hilo kuibwa jana na watu ambao hawajajulikana.
Mkuu wa wilaya hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wilayani humo, Nyabaganga Talaba alithibisha kuwa kamera mbili na viegesho vyake, vyenye thamani ya shilingi milioni 6 vilivyokuwa vikitumika katika zoezi hilo vilipotea mapema asubuhi.
“Ofisa wa Nida alibaini kuwa kamera mbili na viegesho vyake hazionekani jana asubuhi,” alisema Mkuu wa Wilaya. “Tunaendelea kufanya uchunguzi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kuwabaini wahusika na kuvipata vifaa hivyo,” aliongeza.
Akizungumzia sakata hilo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Stephen Magoiga alisema kuwa vifaa hivyo vilikuwa vimehifadhiwa katika ofisi za halmashauri hiyo kabla ya kutoweka.
Naye Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga, Muliro Muliro alisema kuwa Jeshi hilo limeshapokea taarifa ya tukio hilo na wameanza kufanya uchunguzi ikiwa ni pamoja na kuwahoji watu kadhaa.