Serikali ya Sudan imewakamata viongozi tisa wa vyama vya upinzani nchini humo kutokana na vuguvugu la maandamano ya kupinga Serikali yanayoendelea.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya nchini humo, mbali na viongozi waandamizi wa upinzani, wengine waliotiwa mbaroni ni pamoja na wanaharakati pamoja na watetezi wa haki za binadamu.

Hata hivyo, viongozi wa Idara ya Usalama wa Taifa na Huduma za Ulinzi wameeleza kutofahamu kuhusu kukamatwa kwa viongozi wa vyama vya upinzani.

Sudan imekuwa katika sintofahamu kwa zaidi ya wiki moja kufuatia maandamano yanayoendelea kupinga utawala wa Rais Omar al Bashir, kufuatia ugumu wa maisha na kupanda kwa gharama za vyakula na mafuta.

Imeelezwa kuwa takribani watu 19 wamepoteaa maisha kutokana na maandamano hayo ikiwa ni pamoja na wanajeshi, kwa mujibu wa takwimu rasimi.

Hata hivyo, watu wanaounga mkono utawala wa al Bashir umeeleza kuwa maandamano hayo yanachochewa na baadhi ya mataifa ya Magharibi ambayo yana mgogoro na Serikali hiyo.

Al Bashir anatafutwa kwa lengo la kufikishwa mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC). Mahakama hiyo ilitoa hati ya kumkamata Machi 14 mwaka 2009 na hati nyingine ilitolewa Julai 12 mwaka 2010.

JPM amtumbua Mkurugenzi aliyetetea kikokotoo cha 25%
Kikokotoo chamuibua tena Bulaya, 'Bora mjiuzulu'