Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa wamelaani mauaji ya watoto wadogo yaliyotokea hivi karibuni mkoani Njombe yakihusishwa na imani za kishirikina wakisema kuwa matukio hayo yanachafua taswira ya mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

Hayo yamesemwa na Katibu wa Umoja wa Vijana wa chama hicho taifa, Raymond Mwangwala pamoja na Katibu wa Mambo ya Nje wa CCM Kanali Mstaafu, Ngemela Lubinga wakiongozwa na mlezi wa chama hicho katika mkoa wa Njombe, Dkt. Frenk Hawasi.

Wakiwa katika Ofisi za chama hicho mkoa wa Njombe eneo la Mjimwema mlezi wa CCM mkoani humo, Dkt. Frenk Hawasi amesema kuwa chama hicho ngazi ya Taifa kinalaani vikali mauaji hayo kwa kuutia doa mkoa huo.

‘’Tunalaani vikali mauaji haya na tunaendelea kuielekeza Serikali iendelee kuchukua hatua kali juu ya mauaji haya ili wahusika wakamatwe na kufikishwa mahakamani, pia tunawataka wananchi hususani wanachama wa CCM waendelee kuwa watulivu katika kipindi hiki ambapo vyombo vya dola vinaendelea kuwasaka wahusika wa mauaji haya’’. amesema Dkt. Hawasi

Aidha, kwa upande wake, Kanali Mstaafu Ngemela Lubinga amesema kuwa wazazi waliopoteza watoto wao ni wananchi wa Tanzania hivyo amewataka wakazi wa mkoa wa Njombe kutoa taarifa za wahusika wa matukio hayo kwa usiri.

Naye Katibu Mkuu Umoja wa Vijana wa CCM Taifa Mwalimu Raymond Mwangwala amesema kuwa mauaji ya watoto wadogo mkoani Njombe ni moja ya eneo lililogusa umoja wa vijana kwakuwa waliofariki ni Chipukizi ambao ni sehemu ya kitengo kinachoigusa UV,CCM.

 

Mkuu wa Majeshi ateta na Kamati ya Ulinzi na Usalama Njombe
Rais wa Misri amrithi Kagame AU