Mali za viongozi wa Umma takribani 500 zimeanza kufanyiwa uchunguzi na kukaguliwa na Serikali ili kubaini viongozi waliojilimbikia mali kinyume cha sheria.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angela Kairuki jijini Dar es salaam, alipokuwa katika uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya kutoa huduma kwa wananchi katika kuadhimisha siku ya maadili ya kitaifa na Haki za binadamu.
Amesema hatua hiyo itahusisha wananchi ambao watataka kuisadia serikali kutoa taarifa za mali za viongozi wanazozifahamu ili kupata ukweli ambapo amesema kuwa watumishi watakao ficha mali zao watakumbana adhabu kali ikwemo kuchukuliwa hatua za kinidhamu.
“Tunahitaji kurekebisha sheria zetu ili kuwabana watu wanaofanya makosa hayo ya rushwa, kwani adhabu za wakati huu hazilingani na makosa ya rushwa ili kukomesha kabisa tatizo hilo”alisema Kairuki.
Aidha, Kairuki amesema kuna changamoto mbali mbali ambazo zinazojitokeza ikiwemo ya wananchi kusita kutoa ushahidi mahakamani kuhusu masuala yanayohusu rushwa.