Virusi vipya vya Corona (Covic-19) vilivyoanzia nchini China vimeripotiwa kufika katika bara la Afrika baada ya Misri kutangaza kuwa wamebaini kuwepo kwa mgonjwa ambaye sio raia wa nchii hiyo.

Wizara ya Afya ya Misri, Ijumaa, Februari 14, 2020 ilitangaza kuwa muathirika aliyebainika kuwa na virusi hivyo hakuwa na dalili zozote za ugonjwa. Hata hivyo, hawakuweka wazi uraia wake.

“Wizara inachukua hatua za kujikinda na inaendelea kufuatilia mwenendo wa mgonjwa huyu ambaye afya yake inaimarika,” msemaji wa Wizara hiyo, Khaled Megahed aliwaambia waandishi wa habari.

Serikali ya Misri imetoa taarifa rasmi kwa Shirika la Afya Duniani (WHO) na imemtenga mgonjwa huyo kwenye hospitali maalum.

Vifo vya watu vinavyotokana na ugonjwa huo hivi sasa vimeripotiwa kuwa ni zaidi ya 1,500 wengi wakiwa nchini China.

Kutokana na kuwepo kwa ushirikiano wa karibu kati ya wafanyabiashara katika nchi za Afrika na China, mifumo ya kudhibiti uwezekano wa kuwepo mlipuko unaotokana na virusi hivyo unaendelea kutiliwa mkazo.

Hivi karibuni, Misri ilipiga marufuku ndege zake kuelekea nchini China hadi itakapoamua vinginevyo.

Uganda ni moja kati ya nchi zilizotangaza rasmi kutopokea wageni kutoka nchini China katika kipindi hiki hadi mlipuko wa virusi vya corona utakapodhibitiwa. Nchi za Afrika Mashariki bado ziko salama na Serikali za nchi hizo zimetoa taarifa rasmi kueleza kuwa hakuna mgonjwa aliyebainika.

Mtoto wa miaka 12 ajiua baada ya kutuhumiwa kuiba Sh 6,000
Baba mbaroni kwa kutelekeza fanilia ya watoto sita