Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara  msimu 2016/17, raundi ya 12 inaendelea kesho kwa michezo sita, ambapo mabingwa watetezi Young Africans ya Dar es Salaam itakuwa mgeni wa Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba ulioko Bukoba mkoani Kagera.

Jijini Dar es Salaam, katika Uwanja wa Uhuru African Lyon itakuwa mwenyeji wa Mbeya City ya Mbeya ilihali Mwadui ya Shinyanga itasafiri hadi Mtwara kucheza na Ndanda Fc kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona wakati Stand United itakuwa mgeni wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye mchezo utaofanyika Uwanja wa Manungu, ulioko Turiani – Mvomero.

Majimaji itakuwa mwenyeji wa Ruvu Shooting ya Pwani kwenye Uwanja wa Majimaji huko Songea. Michezo yote mitano hapo juu itaanza saa 10.00 jioni kwa saa za Afrika Mashariki lakini mchezo kati ya Azam FC na JKT Ruvu itaanza saa 1.00 usiku kwenye Uwanja wa Azam huko Chamazi-Mbagala Dar es Salaam.

Jumapili itakuwa ni zamu ya kinara wa ligi hiyo, Simba ambayo itaikaribisha Toto Africans ya Mwanza kwenye Uwanja wa Uhuru wakati Tanzania Prisons itapambana na Mbao FC kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Michezo yote ya Dar es Salaam, mfumo wa kuingia utabaki kuwa ni uleule wa kutumia kadi za Selcom kununua tiketi za kielekroniki. Viingilio kwenye mechi za Uwanja wa Uhuru ni Sh 30,000 kwa Jukwaa Kuu (VIP-A), VIP-B na C Sh 20,000 na mzunguko ni Sh 5,000 wakati Kiingilio Uwanja wa Azam ni Sh 10,000 kwa VIP na Mzunguko ni Sh 3,000.

Video: 'Mikutano ya Yanga ni yakihuni' - Mzee Akilimali
TFF: Wadhamini Bado Wana Nafasi Katika Ligi Ya Wanawake