Tukio la furaha la kuwafungisha pingu za maisha wapendanao katika Kanisa la St. James ACK, Kiambu nchini Kenya limeripotiwa kugeuka uwanja wa vurugu baada ya Bwana Harusi kudaiwa kuwa ni mume wa mtu.

Kwa mujibu wa Citizen, tukio hilo limetokea leo, Aprili 27 kanisani hapo baada ya timu ya watu wanaoaminika kuwa ni wafuasi wa mke wa ndoa wa bwana harusi huyo walipofika kanisani na kuharibu shughuli.

Imeripotiwa kuwa bwana harusi huyo alikuwa ameoa tayari lakini walitengana na mke wake kwa muda mrefu. Hata hivyo, imeelezwa kuwa bwana harusi huyo alikuwa hajatalakishana na mkewe na kesi ya madai ya talaka bado haijatolewa uamuzi na mahakama.

Mwandishi wa The Citizen, Charles Gikunga aliyekuwa kwenye eneo la tukio ameeleza kuwa ni kama timu ya bibi harusi ilipata taarifa za ‘kiintelijensia’ kuwa mke wa bwana harusi angekuja kuharibu shughuli hivyo alikodi timu iliyoimarisha ulinzi mkali.

Walinzi hao ndio waliofanikiwa kuwazuia waandishi wa habari kupiga picha nzuri wakati wa tafrani hiyo.

Citizen imeripoti kuwa mmoja wa waandishi wao wa habari aliyejaribu kupiga picha wakati wa varangati alipata majeraha madogo na kuondolewa katika maeneo ya kanisa hilo.

Ndoa za imani ya Kikristo hufungwa kati ya mwanaume mmoja na mwanamke mmoja, na kiapo huwa ni “aliyekiunganisha Mungu binadamu asikitenganishe.” Hata hivyo, kiapo hicho hugeuka msumari kutokana na masharti magumu ya kupata talaka kwa imani ya Kikristo.

Kauli ya Diamond yachochea vita kuu ya Zari na Mange, wararuana
Dkt. Bashiru awazungumzia Nape, Bashe asema ni ‘watukutu, wadadisi’