MWENYEKITI wa Bodi ya Taifa ya Misamaha kwa Wafungwa (Parole) Dkt. Augustine Mrema amevitaka vyombo vya usimamizi wa sheria nchini kutoa adhabu mbadala ya kifungo cha nje kwa wahanga wa matumizi ya dawa za kulevya nchini.

Hatua hiyo inaeelezwa itawezesha kuwapatia huduma bora za matibabu ambazo ni ngumu kuzipata pindi wawapo mahabusu au wakitumikia kifungo katika magereza.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam, Mrema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour Party (TLP) alisema katika siku za hivi karibuni kumezuga tabia kwa baadhi ya askari polisi kuwageuza mtaji wahanga wa madawa ya kulevya.

“Natoa wito kwa Jeshi la Polisi kuacha mara moja tabia ya kuwabambikia kesi wahanga hawa na badala yake washughulike na wakubwa wa wauza madawa hayo ambao wapo katika jamii na wanafahamika na hata baadhi ya Polisi,” alisema Dkt. Mrema.

Aidha Mrema alisema idadi ya watumiaji wa madawa ya kulevya imekuwa ikiongezeka kila kukicha nchini hatua inayoisababisha Serikali kuwa mzigo mkubwa katika kuwahudumia ikilinganisha na mahitaji yaliyopo.

Katika barua yake aliyoiwasilisha kwa Rais, Dkt Mrema alisema wahanga hao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa vituo vya tiba, kutengwa na kukamatwa mara kwa mara na polisi.

Kwa mujibu wa Mrema alisema ndani ya barua hiyo pia amemshauri Rais John Magufuli kuwasaidia wahanga hao kupata maeneo maalum ya mashamba kwa ajili ya kuendesha shughuli za kilimo ili makundi hayo yaweze kujiongezea kipato.

Dkt Mrema pia aliishauri Serikali kuwapa wahanga hao jukumu la kusafisha Jiji la Dar es Salaam na kuwa walinzi wa wachafuzi wa mazingira.

“Faini iliyopangwa na jiji ni Tsh. 50,000, kati ya hizo nashauri tsh 20,000 wapewe wahanga hawa ili iwe kama motisha kwao” alisema Dkt Mrema.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa magonjwa ya akili kutoka hospitali ya taifa muhimbili, Dkt. Cassian Nyandindi jamii haina budi kubadili mtizamo kuhusu watumiaji wa madawa ya kulevya, kwa kuwa wahanga hao hawakupenda kuwa wategemezi katika matumizi ya madawa hayo.

Dkt. Nyandindi alisema hospitali hiyo kwa kwa sasa imekuwa ikikabiliwa na changamoto kubwa ya kuwahudumia wahanga wa matumizi ya dawa za kulevya ikiwemo uhaba wa watumishi pamoja na vituo vya kutolea huduma.

Dkt. Mrema ameeleza kuwa vijana hawa walipokuwa wakituia dawa za kulevya walidhalilika katika jamii na kuonekana kama wanyama na kupelekea hata jamiii kuwatenga kutokana na vitendo vya uhalifu lakini baada ya kuanza matibabu wamebadilika kitabia na hata jamii imeanza kurudisha imani kwao.

Akielezea kero wanazokutana nazo Dkt. Mrema amesema kuwa wahanga wengi wamekuwa wakikamatwa na Polisi kwa kukutwa na kete moja au mbili na kufunguliwa mashtaka mahakamani.

“Nimetoa ushauri badala ya kuwapeleka magerezani wasioanza tiba bali wapelekwe hospitalini na waanzishiwe tiba ili kuwarejesha katika utu wao,” alisema Dkt. Mrema.

Msanii Kutoka Nigeria YCEE Atoa Msaada Kituo Cha Kulelea Watoto Wanaoishi Katika Mazingira Magumu Kigamboni Community Center
Mwanasheria Mkuu Avitaka Vyama Vya Siasa Kufuata Misingi Ya Katiba, Sheria Na Busara