Waandaaji wa tuzo za Oscar, The Academy of Motion Picture Arts and Science wamewafukuza kwenye jopo lake, Muongozaji wa filamu Roman Polanski na Bill Cosby kwa tuhuma za unyanyasaji wa kingono na ubakaji.

Bodi ya taasisi hiyo ilikutana Juamnne usiku na kupiga kura ambayo ilisababisha wawili hao kuondolewa rasmi kwenye uanachama.

Cosby alikutwa na hatia katika makosa matatu ya unyanyasaji wa kingono Aprili 26 kwa kumlazimisha Andrea Constand kuingia ndani ya jumba lake la kifahari la Philadelphia na kumnyanyasa kingono mwaka 2004.

Kutokana na kukutwa na hatia, anakabiliwa na kifungo cha hadi miaka 30.

Kwa upande wa Polanski mwenye umri wa miaka 84 ambaye alienda Ufaransa kwa ajili ya mambo yake binafsi, anatafutwa na Marekani ili ajibu tuhuma za kumbaka msichana mwenye umri wa miaka 13, kitendo anachodaiwa kukifanya mwaka 1977.

 

Vigogo hao kwenye kiwanda cha filamu wanadaiwa kufanya makosa ya kuwanyanyasa waigizaji wa kike kingono kwa kutumia nafasi zao, wakiwaahidi kuwa watawainua na kuwafanya wawe maarufu.

Mwaka jana, waandaaji wa tuzo za Oscar walipiga kura kumuondoa nguli wa filamu, Harvey Weinstein kutokana na tuhuma za kufanya unyanyasaji wa kingono kwa waigizaji kadhaa wa kike.

Lupita Nyong’o ni mmoja kati ya waigizaji waliojitokeza kuanika unyanyasaji wa kingono aliofanyiwa na waliokuwa na nguvu katika kiwanda cha filamu miaka kadhaa iliyopita, hali iliyowaweka hatiani.

 

Msigwa aomba radhi kwa kumwagia sifa Rais JPM
Ommy Dimpoz aweka wazi wanaomuomba awaoe