Baadhi abunge wa ngome za Jubilee na National Super Alliance (NASA), wamemshauri kiongozi mkuu wa ngome ya upinzani, Raila Odinga kuachana na siasa za Kenya ili aweze kujikita katika kazi mpya aliyoteuliwa ya Umoja wa Afrika.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwenye tukio la kuchangisha fedha za maendeleo katika jimbo la Kesses, wabunge hao wamesema kuwa kazi mpya aliyopewa Raila inamtaka awe na muda mwingi zaidi kuikamilisha, hivyo anapaswa kuachana na siasa za nyumbani.

Kati ya wabunge 18 waliounga mkono ajenda hiyo, ni pamoja na Ndindi (Kiharu), Kimani Ichungwa (Kikuyu), Didmus Barasa (Kimilili) na Oscar Sudi (Kapsaret).

“Kwa sababu hivi sasa ana kazi kubwa zaidi ya kuitumikia Afrika nzima, anapaswa sasa kuachana na siasa za hapa nyumbani,” mbunge wa Nyoro alisema. “Aina ya kazi aliyopewa hivi saa haimruhusu kushiriki kikamilifu kwenye siasa za nyumbani,” aliongeza.

Mbali na wabunge hao, Seneta wa Kakamega, Bonny Khalwale aliounga mkono hoja hiyo akidai kuwa hivi sasa Raila anapaswa kujikita zaidi katika kuwaandaa vijana kuchukua nafasi yake.

“Mzee haruhusiwi kucheza na vijana, Raila amecheza na Matiba, Moi na Kibaki, anatakiwa kuacha hivi sasa kwakuwa muda wake umekwisha,” alisema Khalwale.

Hata hivyo, wakati hoja hiyo ikisukumwa kwa nguvu, bado joto la kugombea urais 2022 linazidi kupanda, Raila akitajwa kuchuana vikali na makamu wa Rais, William Ruto.

Mwanasiasa huyo mkongwe ameteuliwa na Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat kama Muwakilishi wa Umoja wa Afrika wa Maendeleo ya Miundombinu Afrika.

Makamba aeleza alivyohojiwa sakata la Mo Dewji, ‘sikukamatwa’
Video: Hii ndiyo ndege inayomilikiwa na familia ya kitajiri ya Qatar