Shirika lisilo la kiserikali mkoani Njombe Youth Development Organization (NJOYODEO) kwa kushirikiana na umoja wa vijana chama cha mapinduzi (CCM) mkoani humo wametoa msaada wa Mashuka na Blanketi kwa wafungwa walioko katika Gereza la Mpechi mkoani humo.

Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Mkuu wa Gereza la mkoa wa Njombe SP Charles Myinga amesema kuwa idadi kubwa ya wafungwa na mahabusu gerezani hapo wanakabiliwa na kesi za mauaji ambazo chanzo chake ni migogoro ya ardhi, ushirikina na tamaa ya utajiri na kuendelea kuisisitiza serikali na mahakama kuongeza nguvu katika usikilizaji wa kesi za mauaji

Amesema kuwa Gereza linakabiliwa na changamoto nyingi hivyo msaada uliotolewa na wadau hao utasaidia kupunguza changamoto licha ya kuwa na uhitaji mkubwa kwa mahabusu,huku jeshi hilo pia likiwa na uhaba wa makazi ya askari.

“Sisi tunatoa shukrani lakini bado uhitaji ni mkubwa na sasa hivi jeshi tunauhaba wa makazi ya askari na kwasasa tunafyatua matofari ya kutosha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari kwa hiyo kama kuna wadau wanaoweza kujitolea kutoa Mabati, Misumari na Mbao, sisi vyote tunapokea lengo letu askari wapate makazi,”amesema Myinga

Kwa upande wake mkurugenzi wa shirika hilo, Hamis Kasapa na Nehemia Tweve ambaye ni mwenyekiti wa umoja wa vijana UVCCM mkoa wa Njombe, wamesema sababu zilizowagusa kutembelea katika Gereza hilo ni uwepo wa idadi kubwa ya vijana waliofungwa pamoja na mahabusu jambo ambalo linaonyesha kundi la vijana ndiyo nguvu kazi ya taifa lakini idadi kubwa wako hatarini kuishia gerezani.

Aidha, wamesema kuwa wao kama vijana hawatoi misaada kwa ajili ya kuwadekeza wafungwa isipokuwa ni kufikisha baadhi ya huduma za msingi ambazo wafungwa wanazikosa.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa Gerezani hapo zaidi ya asilimia 70 ya wafungwa wake na mahabusu ni vijana na wana kabiliwa na kesi za mauaji.

Krepin Diatta alamba shavu
Video: Kiburi champonza Lissu, Serikali kuboresha mfumo wa biashara