Leo Julai 24, 2018 Kamanda wa Polisi Kanda maalumu ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa amesema Jeshi la polisi linawashikilia watuhumiwa wawili kwa tuhuma ya kuhujumu kampuni ya mawasiliano Tanzania ya (TTCL) na kusababisha shirika hilo kupata hasara ya shilingi milioni 46 za kitanzania.

Mambosasa ametaja watuhumiwa hao kuwa ni Kelvin Siame (25) mkazi wa Tabata Segerea ambaye ni mfanyakazi wa shirika hilo kitengo cha huduma kwa wateja na mwingine ni Lilian Hosea (36), mkazi wa Mbezi Beach ambaye alikuwa ni mhasibu wote wakiwa ni wafanyakazi wa TTCL.

”Mnamo julai 12, 2018, Jeshi la polisi kanda maalumu  lilipata taarifa kutoka kwa Afisa mpelelezi kampuni ya mawasiliano ya TTCL kuwa wafanyakazi wa shirika hilo wanajihusisha na udukuzi wa data za kampuni ya TTCL kutoka Taasisi za Serikali zinazotumia mtandao huo na taasisi hizo ni UDSM, TASAF, NSSF, NHC na TRA”. amesema Mambosasa.

Ameongezea kuwa Taasisi hizo zilikuwa zikinunua data toka kampuni ya TTCL kwa ajili ya matumizi ya kila siku, lakini watumiwa hao wamekuwa wakiiba data hizo na kuwauzia watumiaji binafsi kwa manufaa yao binafsi na kusababisha shirika kupata hasara kubwa ya fedha.

Mara baada ya watuhumiwa hao kutiwa mbaroni na kufanyiwa mahojiano ya kina walikiri kuhusika na uhujumu huo kwa kuuza data kinyume na sheria.

Aidha taratibu zinafanyika ili watuhumiwa hao waweze kufikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kuwa umekamilika.

 

Besiktas kumng'oa David Ospina Emirates Stadium?
'Mahakama imezingatia maelezo ya kukiri kosa mauaji ya bilionea Msuya ' Jaji Maghimbi