Wakazi wa Wilaya ya Njombe mkoani Njombe wameaswa kuhamasika kupima kansa ya mlango wa kizazi ili kupunguza vifo vya wanawake waliokuwa wakipoteza maisha yao kutokana na kuchelewa kupelekwa hospitali kwa sababu za imani za kishirikina.
Rai hiyo imetolewa kwenye uzinduzi wiki ya chanjo ya mlango wa kizazi kijiji cha Nyombo, Kata ya Ikuna na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, Valentino Hongoli ambapo amesema wanawake wengi Wilayani humo wamepoteza maisha kutokana na kuamini wamerogwa imani ambayo kwa sasa wanapaswa kupingwa.
“Achaneni na imani za kishirikina fanyeni vipimo ili kugundua matatizo mapema…, tatizo hili ni kubwa limeua wakinamama wengi ambao walikua wakiumwa na kwenda kwa waganga wa kienyeji”amesema Hongoli.
Akisoma taarifa ya uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, Monica Kwiluhya amesema wasichana zaidi ya 1600 wanatarajiwa kupatiwa chanjo hiyo.
Mkurugenzi huyo amesema kuwa wanaelimisha jamii kupitia vyombo mbalimbali vya habari ikiwemo redio na Televisheni ili walengwa ambao ni wasichana kujitokeza kwa wingi.
Mgeni rasmi katika uzinduzi huo, Katibu Tawala Wilaya hiyo, Jafari Simika amesema chanjo hiyo inapaswa kuelezwa bila woga katika taasisi mbalimbali ikiwemo Makanisa na Misikiti.

Kocha Mwinyi Zahera atua Tanzania, azungumza na Young Africans
Waziri Ummy azindua ugawaji wa vyandarua vyenye dawa ya muda mrefu Kigoma