Zaidi ya wakazi 1000 wa Kanda ya Ziwa wamenufaika na matibabu ya bure hasa kwa upande wa upasuaji unaofanywa na Chama cha Madaktari wa Upasuaji Tanzania.

Hayo yamesemwa na Rais wa Chama cha Madaktari wa Upasuaji Tanzania, Dkt. Catherine Mung’ong’o wakati wa siku ya kuhitimisha zoezi la upasuaji lililofanyika kwa siku tano kuanzia tarehe 03 hadi 07 Juni 2019 katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza.

Amesema kuwa lengo la upasuaji huo ni kupunguza idadi ya wahitaji wa huduma ya upasuaji kwa wagonjwa wanaosubiri kwa muda mrefu toka Kanda ya Ziwa, na kuongeza kuwa zoezi hilo limefanyika kwa ushirikiano baina ya Chama hicho, Madaktari wa Hospitali ya Rufaa ya Bungando na Madaktari wengine.

Aidha, Dkt. Mung’ong’o  amesema kuwa huduma hiyo ya upasuaji inayotolewa na Chama cha Madaktari wa Upasuaji Tanzania imekuwa ikifanyika kila mwaka katika mikoa mingine huku ni ikiwa ni mara ya kwanza katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Kwa upande wake Kiongozi wa Chama hicho Kanda ya Ziwa ambaye ni Daktari Bingwa wa Upasuaji toka Hospitali ya Rufaa Bugando, Dkt. Olivia Kimario amesema kuwa zoezi hilo ni utaratibu uliowekwa na Chama cha Madaktari hao ambapo mwaka huu wamehudumia katika mikoa ya Mwanza , Shinyanga , Mara na Geita.

Katika hatua nyingine Dkt. Mung’ong’o ameongeza kuwa baada ya kukamilisha zoezi hilo la upasuaji kwa wagonjwa wanaosubiri kwa muda mrefu, Chama hicho kitatoa huduma bure za upasuaji kwa wagonjwa wenye matatizo ya Mdomo Sungura litakalofanyika tarehe 10 na 11 Juni 2019 bila ya malipo.

Lema asema kauli ya JPM inaleta matumaini
Rais wa Uturuki asimamia ndoa ya Ozil