Wananchi wa Kijiji cha Korinto Kata ya Luduga Wilaya ya Wanging’ombe Mkoani Njombe wamewaeleza viongozi wa chama cha mapinduzi CCM mkoa wa Njombe tatizo la uhaba wa walimu linalozikabili baadhi ya shule katika kata yao.

Wakizungumza na viongozi hao ambao ni Katibu wa CCM Mkoa wa Njombe, Paza Mwamlima, Katibu wa siasa na uenezi mkoa, Erasto Ngole pamoja na katibu wa idara ya wazazi mkoani humo, Lucas Nyanda waliofika kufanya mazungumzo na wanachama wa chama hicho katika kata ya Luduga.

Wakorinto hao wamewaeleza kuwa baadhi ya shule katika kata yao zinakabiliwa na tatizo la uhaba mkubwa wa walimu ikiwemo shule ya msingi Korinto.

Akizungumza kwa niaba ya viongozi wengine Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM mkoa wa Njombe, Erasto Ngole amewaeleza wananchi hao kuwa chama kimepokea tatizo hilo hivyo uongozi utafanya mawasiliano na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wanging’ombe ili kuona namna ya kupunguza tatizo hilo.

“Ndg. Wananchi wa Kata ya Luduga pamoja na wananchi wa Korinto niwaeleze kuwa chama kimeshaichukua changamoto hiyo naahidi kuwa tunaenda kuifanyia kazi kikubwa Mh. diwani hakikisha kuwa unatuletea orodha ya shule zilizopo ndani ya kata yako ambazo zina upungufu mkubwa wa walimu,”amesema Ngole

Aidha, katika hatua nyingine Wakorinto hao walipokea maelekezo ya kuimarisha chama kutoka kwa katibu wa CCM mkoa wa Njombe, Paza Mwamlima aliyewasisitiza kujiandaa na uchaguzi wa serikali za mitaa ambao utafanyika mwaka huu.

Hata hivyo, Ngole amewakabidhi viongozi wa CCM Kata ya Luduga walioshiriki kikao hicho pesa kiasi cha Tsh.100,000/= kwa ajili ya chakula akisema kuwa anatambua kazi kubwa wanayoifanya ndani ya chama kwakujitolea huku viongozi hao wakieleza kuwa kiongozi huyo ni mtu wakujitoa kusaidia wengine ndani na nje ya CCM.

Zimbabwe yazima mitandao ya kijamii kuzima maandamano
Uganda: DJ auawa kwa kucheza muziki mbaya