Kukosa tija na masoko ya zao la mahindi kumeelezwa kuwa ni miongoni mwa sababu zilizo wapelekea baadhi ya wakulima mkoani Rukwa kutangaza kususia kilimo cha mahindi ambalo ni zao linalolimwa mkoani humo kwa muda mrefu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakulima hao wamesema uamuzi huo wameufikia kutokana na kukosa bei ya mazao hayo na hivyo kujikuta wakikabiliwa na ugumu wa maisha kwa kukosa fedha za kuendesha maisha yao.

Mmoja wa wakulima hao, Peter Shinyangwe mkazi wa kijiji cha Kalumbaleza wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa amesema haoni umuhimu wa kulima mazao ya chakula kwakuwa hayana soko na hakuna mipango yoyote inayofanywa na Serikali kuwasaidia ili waweze kupata soko.

Aliongeza kuwa pamoja na gharama kubwa za uzalishaji wa mazao hayo ikiwemo pembejeo za kilimo lakini wanaishia kuuza gunia la mahindi la kilogramu miamoja kwa bei ya sh. 20,000 kitendo kinachowakatisha tamaa kwa kuto kuona faida ya kulima mazao hayo.

Naye Adrian Kashamakula, mkazi wa Kantawa wilayani Nkasi ameongeza kuwa ‘’Hali hii imetukatisha sana tamaa wakulima na nina amini wengi hawatalima tena kwakuwa hawana fedha za kununulia pembejeo  na hawajui soko la mazao yao,kwakuwa mazao ya chakula hayana msaada tofauti na mazao ya biashara kama korosho’’,  amenukuliwa na Mtanzania

Aidha, hivi karibuni katika kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa wa Rukwa chini ya mwenyekiti wake Mkuu wa mkoa, Joachim Wangabo, ameagiza maofisa ugani kuhakikisha wanakuwa karibu na wakulima na kuwapa mbinu za kulima kisasa ili waongeze mavuno.

Mtanzania akamatwa na dawa za kulevya Kenya
Fiesta yasitishwa Dar, "Tunaomba radhi kwa masikitiko makubwa"