Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Suleiman Jafo amewapa muda wa siku 14 wakurugenzi wa halmashauri zaidi ya 40 nchini kuwasilisha barua ya kujieleza ni kwa nini wasichukuliwe hatua kwa kupeleka asilimia 10 ya wanawake, vijana na walemavu chini ya asilimia 50 ya mapato yao.

Ameyasema hayo jijini Dodoma alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa wakurugenzi hao wa halmshauri watapaswa kuandika barua kwenda kwa katibu mkuu wa TAMISEMI ndani ya wiki mbili wakijieleza kwa nini wasichukuliwe hatua kwa kuvunja sheria.

Agizo hilo linaenda pia kwa halmashauri zilizofanya vibaya katika ukusanyaji wa mapato kwa kukusanya chini ya asilimia 50 ya malengo waliyojiwekea.

Aidha, Jafo ameyapongeza majiji 6 kwa kukusanya vizuri mapato kiasilimia wakiongozwa na jiji la Arusha lililokusanya asilimia 105 huku jiji la Dodoma likiongoza kukusanya shilingi bilioni 71.727 kama pato ghafi .

Pia ameongeza kuwa kukusanya mapato ni jambo moja na kuhakikisha mapato hayo yanaenda kwa wananchi kupitia miradi ya maendeleo ni jambo la pili na hivyo kulitaja jiji la Dodoma pekee kupeleka asilimia 75 ya mapato yake kwa wananchi.

Mbali na hayo ameweka bayana zawadi maalum ya vinyago itakayotolewa kwa halmashauri zilizofanya vibaya katika ukusanyaji wa mapato kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019.

LIVE IKULU: Rais Magufuli akizungumza na Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa
Rufaa ya Bageni yagonga mwamba, kunyongwa hadi kufa