Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimetoa siku 15 kwa Serikali kumaliza madai yao ya muda mrefu vinginevyo watachukua maamuzi magumu.

Rais wa CWT, Gratian Mukoba amesema kuwa uvumilivu wao umeelekea kufikia ukingoni kwani wamekuwa wakikaa mezani na Serikali mara kwa mara na kupewa ahadi za kutatua matatizo yao lakini hadi sasa hazijatekelezwa.

Alisema kuwa Agosti  22 na 23 mwaka huu, Baraza la chama hicho cha walimu lilipitisha maazimio kupitia kikao chake, maazimio ambayo yalisainiwa pia na upande wa Serikali kwa ahadi kuwa wangeyafanyia kazi lakini imeendelea kuwa kimya.

“Siku chache baadae tuliambiwa tusubiri mchakato wa kuhakiki watumishi ukamilike. Lakini licha ya mchakato huo kukamilika Serikali imeendelea kukaa Kimya,” Mukoba anakaririwa na Tanzania Daima.

Aliyataja madai hayo kuwa ni pamoja na posho ya madaraka kwa wakuu wa shule, muundo wa madaraka, walimu kutopandishwa madaraja na kulipa madeni ya walimu.

“Ninachoweza kukwambia ni kwamba mwishoni mwa Oktoba ambao umebakiza siku 15 tutachukua uamuzi mzito ambao haujawahi kutokea na hatutaki lawakama kutoka sehemu yoyote ile,” alisema Mukoba.

Rais huyo wa CWT alidai kuwa ingawa Serikali imepiga hatua katika sera ya elimu bure na madawati, lakini mazingira ya walimu na ufundishaji yameendelea kuwa magumu hivyo ni vigumu kupandisha ubora wa elimu.

Hatari: Mwanafunzi wa shule ya msingi adai alijifunza kulawitiwa toka kwa wazazi wake
Mashabiki wa Coastal Union wamshushia refa kipigo cha mwizi!