Serikali imetoa ufafanuzi kuwa Watanzania waliokamatwa Malawi siyo majasusi, bali ni wafanyakazi wa taasisi ya CARTAS ya Songea, iliyopo chini ya Kanisa Katoliki.
Hayo yamebainishwa mara baada ya kufanya ufuatiliaji ambapo imebainika kuwa ni kweli watanzania wanane kutoka taasisi ya CARTAS iliyopo chini ya kanisa katoliki Songea, Mkoani Ruvuma, walikamatwa na Vyombo vya Usalama katika Wilaya ya Karonga ambayo inapakana na Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya, na kufuguliwa mashtaka kwa kosa la jinai la kuingia eneo la Mgodi bila kibali.
Aidha, taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imefafanua kuwa baada ya kupata taarifa ya kukamatwa kwa watanzania hao, Ubalozi ulifika pale walipokuwa wanashikiliwa na kujua kwamba walienda kwaajili ya ziara ya mafunzo ambapo walitaka kujua madhara yatokanayo na machimbo ya urani.
Hata hivyo taarifa hiyo imefafanua kuwa Ubalozi unaendelea kufanya mawasiliano na kanisa Katoliki Songea kwa lengo la kupata maelezo zaidi kuhusu ziara ya watu hao, kwa madhumuni ya kuyawasilisha kwa mamlaka husika ili watuhumiwa waweze kutolewa.
Watanzania hao kwasasa bado wanashikiliwa katika Gereza Kuu la Mzuzu hadi kesi yao itakapotajwa tena Januari 4, 2017.