Kundi la watu wenye silaha ‘Wasiojulikana’ waliomteka Padri wa Kanisa Katoliki la Mt. Paulo, Parokia ya Karambi, Goma nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wametoa sharti la kulipwa $500,000 ili wamuachie huru mtumishi huyo.

Watu hao wenye silaha walimteka Fr. Celestin Ngango saa chache baada ya kumaliza kuongoza ibada ya Sikukuu ya Pasaka katika kanisa hilo.

“Waliomteka wamewasiliana na Kanisa la Mt. Paulo, Parokia ya Karambi wakitaka $500,000 kama malipo ya kumuachia huru,” imeeleza taarifa ya Baraza la Maaskofu wa jimbo la Kivu Kaskazini na Kusini.

Majimbo ya Kivu Kusini na Kaskazini yamekuwa yakikumbwa na mashambulizi ya watu wenye silaha na vikundi vya waasi ambao hufanya unyang’anyi na vitendo vingine vya kihalifu dhidi ya raia.

Vikundi hivyo vya waasi vimejikita katika eneo hilo vikipambana kudhibiti maeneo yenye madini mbalimbali.

Wachungaji watatu waliwahi kushikiliwa Oktoba 2012, na wengine wawili waliwahi kutekwa Julai mwaka jana. Baraza la Maaskofu limeeleza kuwa hakuna taarifa yoyote kuhusu watumishi hao wa Mungu tangu walipopotea.

Mbunge mwanamke awaomba wanaume waoe wanawake wengi
Ronaldo aendelea kuwanyamazisha Juventus