Wanafunzi wa kike na walimu katika shule moja ya bweni iliyoko kaskazini mashariki mwa Nigeria, wamefanikiwa kuwatoroka magaidi wa Boko Haram waliokuwa na mpango wa kuwashambulia.

Mashuhuda  wa tukio hilo wameviambia vyombo vya habari kuwa jana jioni wapiganaji wa Boko Haram walifika katika mji wa Dapch jimbo la Yobo wakiwa na gari aina ya pick-up na kisha kuanza kufyatua risasi na kutega mabomu.

Baada ya kusikia milio ya risasi, wanafunzi, walimu na wafanyakazi wengine wa shule hiyo walianza kukimbia kukwepa mkono wa magaidi hao.

Aprili 2014, Boko Haram waliwateka wanafunzi wa kike 270 kaskazini mashariki mwa mji wa Chibok.

Wakaazi wa eneo la Dapch wanaamini kuwa Boko Haram walitaka kufanya utekaji mwingine wa wanafunzi wa kike jana.

Baada ya kufika na kukuta shule haina watu, Boko Haram waliharibu majengo ya shule hiyo. Jeshi la Nigeria likitumia ndege ya kivita lilifika katika eneo hilo na kuzima mashambulizi hayo.

Video: Machozi ya Akwilina, Mbowe na vigogo sita waitwa polisi
Trump ataka sheria ya umiliki wa silaha ifanyiwe marekebisho