Wanafunzi watano waliokuwa wanafanya mitihani ya kuhitimu kidato cha nne katika Kaunti ya Murang’a nchini Kenya, jana walikamatwa wakiwa na simu za mkononi ndani ya chumba cha mtihani.

Wanafunzi hao wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Kiislam ya Murang’a’, walikamatwa wakiwa wanaendelea kufanya mtihani wa Fizikia (physics), kwa mujibu wa polisi.

Imeripotiwa kuwa wanafunzi hao walikamatwa baada ya maafisa usalama kutoa taarifa Polisi kuwa wamebaini kuna vitendo visivyo vya kawaida vinavyoendelea katika kituo hicho cha mitihani.

Baada ya kufanya upekuzi wa kina kwenye shule hiyo, walifanikiwa kuwakamata wanafunzi hao wakiwa na simu. Walipelekwa katika kituo cha Polisi cha Murang’a ili kueleza kwa namna walivyoruhusiwa kuingia na simu ndani ya chumba cha mtihani.

Mkuu wa Polisi wa Murang’a amesema kuwa mwalimu mkuu wa shule hiyo pamoja na msimamizi wa mitihani pia wamefikishwa kituoni hapo kutoa maelezo.

Alisema kuwa pamoja na hatua nyingine, msimamizi wa mitihani ataondolewa mara moja na hataruhusiwa kamwe kusimamia mitihani.

Diamond amvuta Wizkid Wasafi Festival
Avamia hospitali na kuua watatu kwa risasi akimlenga mpenzi wake