Wananchi wa Kijiji Cha Wangama Wilayani Wanging’ombe Mkoani Njombe wameiomba serikali kuwasaidia kukamilisha wodi ya wanaume inayojengwa katika zahanati ya kijiji hicho ambayo bado haijakamilika ili iweze kupunguza changamoto ya wagonjwa wa kiume wanapohitaji kupumzishwa huku zahanati hiyo ikiandaliwa kuwa kituo cha afya.

Akisoma katika taarifa ya Kijiji hicho Afisa Mtendaji wa Kata ya Wangama, Upendo Fute Mbele ya Mbunge wa Jimbo la Wanging’ombe Aliyefanya ziara katika Kijiji hicho ameeleza Kuwa Wananchi na Serikali wamejenga Wodi ya Wanaume lakini bado Kukamilisha ukarabati kutokana na kuishiwa fedha.

“Kuhusu afya zahanati ya Wangama imejenga jengo la wodi ya wanaume ambalo bado kumalizia sakafu chini ,madirisha, mirango na vitendea kazi vyenye thamani ya shilingi milioni kumi na moja, lakini wananchi wamefyatua tayari matofari kwa ujenzi wa maabara kama maandalizi ya kuwa kituo cha afya”amesema Fute

Kwa upande wake, mbunge wa Jimbo la Wanging’ombe mhandisi, Gerson Lwenge amewataka wananchi hao Kuendelea kuchangia ukarabati wa wodi hiyo huku akiwaunga mkono kwa Kuwachangia fedha kiasi cha shilingi milioni moja.

Nao baadhi ya wananchi wa kijiji hicho waliokuwa wamehudhuria mkutano huo wamesema kuwa wamekuwa wakiteseka kwa kusafiri umbali mrefu kwenda Kituo cha afya Kidugala au hospitali ya Ikonda wilayani Makete pamoja na kutumia gharama kubwa pindi wagonjwa wanapozidiwa na kutakiwa kulazwa kutokana na Kutokamilika Kwa wodi la wanaume na endapo litakamilika Litawasaidia Kupata huduma za matibabu Karibu.

 

Gardner amzungumzia Kibonde ‘tusiyemjua’
Elimu yatajwa kuwa kikwazo kwa viongozi wa vyama vya ushirika