Serikali imetoa siku nne kwa wanunuzi wote 35 waliojiandikisha kununua korosho wawe wamepeleka barua katika Ofisi ya Waziri Mkuu wakionyesha kiasi cha tani wanazohitaji na lini watazichukua.

Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa wakati akitoa tamko la serikali kuhusu ununuzi wa zao la korosho.

Amesema kuwa kwenye msimu wa ununuzi wa Korosho wa mwaka huu, walishuhudia kusuasua kwa minada ambapo serikali ilikutana na wanunuzi wa zao hilo katika kikao kilichoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli na kukubaliana kununua kwa bei isiyopungua shilingi 3000.

“Mwenye nia ahakikishe katika siku hizo nne iwe ndio mwisho wa kununua korosho na waandike barua kwani ofisi yangu ipo wazi saa 24 wana nafasi ya kuleta barua wakati wowote wakionyesha nia yao na kiwango wanachohitaji, zaidi ya hapo serikali haitaruhusu kampuni yoyote kununua korosho tena”, amesema Majaliwa.

Aidha, amesema kuwa baada ya kupita siku hizo serikali italazimika kufuta usajili kwa wafanyabiashara wote waliojisajili kununua zao hilo kwasababu walikubaliana kwenda kununua lakini hali inayoonekana sasa ni kama kumkomoa mkulima.

Akizungumza na wanunuzi wa korosho Oktoba 28, Rais Magufuli alimuagiza Waziri mkuu kusimamia manunuzi ya zao hilo kabla ya kulisimamia yeye maana anaweza kumuondoa endapo akishindwa.

 

 

Klabu bingwa Afrika: Simba SC kuanza na Waswaziland
Raia wawili wa Kichina watupwa jela