Taasisi ya kupambana na kuzuia rushwa nchini, TAKUKURU imeingilia kati sakata la kuingizwa vichwa 11 vya treni kinyemela ambapo uchunguzi zaidi unafanyika kubaini waliohusika na sakata hilo.

Siku tisa zilizopita Rais Magufuli alifanya ziara katika ofisi za Makao Makuu ya Takukuru na kuagiza kuchukua hatua dhidi ya tuhuma mbalimbali za rushwa ikiwemo sakata la vichwa 11 vya treni vilivyopo Dar es salaam.

”Kuna mambo mengi ya ovyo yanafanyika, tumebaini wafanyakazi hewa zaidi ya 19500, tumebaini kaya maskini hewa 56,000 zilizopaswa kupata fedha TASAF, tumebaini wanafunzi hewa 5,850 waliotakiwa kupata mkopo, kuna vichwa vya treni 11 vimeletwa bila kuwapo mkataba na mengine mengi, haya yote yanafanyika kwa rushwa, nataka kuwaona mnachukua hatua stahiki.” amesema JPM.

Ameongeza kwa kusema kuwa ”Kwa taarifa yenu TPA, ninajua kuna vichwa vya treni mmevipokea na hamjui ni vya nani na vinaenda wapi, na TRL wamevikana, na meli iliyoshusha imeshaondoka na nyie hamna  nyaraka yoyote ile ya mzigo”.

Hayo yalizungumwa na Rais JPM, katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi la mradi wa uboreshaji wa Bandari ya Dar es salaam wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 421 ambayo ni sawa na sh.bilioni 926.2 za kitanzania.

Hivyo imeelezwa kuwa wote waliohusika katika kuagiza vichwa hivyo wataumbuka baada ya majina yao kuwekwa wazi na kufikishwa katika mikono ya sheria.

Hivyo ameviagiza vyombo vya dola kutafutia ufumbuzi wa suala hilo.

 

 

Dawa za kuongeza nguvu za kiume zapigwa marufuku
LIVE BREAKING: Kamati ikitoa taarifa ya uchunguzi wa madini ya Tanzanite, Almasi