Wafanyabiashara na Wasafirishaji wa Dawa za kulevya aina ya Mirungi wamekuja na mbinu mpya ya kujigeuza kuwa wanafunzi na kisha kuficha Mirungi katika mabegi madogo yanayotumiwa na wanafunzi kuhifadhi Daftari kwa lengo la kukwepa mkono wa Askari Polisi.

Mbinu nyingine ambazo zimezigundulika hivi karibuni ni pamoja na kutumia magari ya Kifahari yakiwemo Toyota Land Cruser ,Toyota Alphasad, Toyota Vanguard huku mbinu nyingine zikiwa ni kufanyia mabadiliko gari aina ya Toyota Noah ili kurahisisha ubebaji wa Mirungi kwa kificho.

Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Kamishna Msaidizi wa Polisi ,Hamis Issah ambapo amesema kuwa wasafirishaji wa Dawa za kulevya aina ya Mirungi wameendelea kubuni mbinu kila kukicha baada ya zile za awali kushtukiwa na Polisi huku akitoa onyo kwa wamiliki wa Magari ya abiria kujiingiza katika mtego wa kusafirisha dawa hizo.

”Hapa kuna mizigo ambayo imekamatwa na askari wetu wakiwa barabarani ,hii ni mbinu mpya ya usafirishaji ,haya mabegi unayo yaona yote ni mabegi yanayoonyesha mbebaji amebeba Madaftari anaenda shuleni ,lakini haya sio madaftari ni Mirungi, ni mizigo iliyokamatwa kwenye mabasi tofauti tofauti,”amesema Kamanda Issah.

Aidha, katika tukio hilo watuhumiwa tisa wakiwemo wanawake wawili wamekamatwa wakiwa na jumla ya kilogramu 64 baada ya sakari Polisi kupekuwa magari matatu ya Abiria yaliyokuwa yakitokea Moshi yakielekea Arusha.

Kamanda Issah amewataja wanaoshikiliwa hadi sasa kuwa ni pamoja na Ibrahim Masuli, Godfrey Richard, Chrispin  Baltazar, Fanuel Hamad na Jackline Mushi huku wengine wakiwa ni Lucy Petro ,Nuru Haruna, Silvesta Fabian naMinyari Miandei.

Hata hivyo, Kamanda Issah amewataka wamiliki wa mabasi ya abiria kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi ili kuhakikisha biashara hiyo inakoma kwa kukataa kubeba abiria wenye mizigo ambayo wanatilia shaka na kwamba kwa kuendelea kuwabeba itapelekea kuwaingiza katika matatizo na vyombo vyao.

Kukamatwa kwa Dawa hizo zinafanya idadi kamili ya Dawa za kulevya aina ya Mirungi zilizokamatwa katika kipindi cha wiki mbili kufikia kilogramu 564 pamoja na vyombo vya usafiri yakiwemo magari matatu na pikipiki moja.

Video: Sura mbili ziara za Lissu nje ya nchi, Bunge latoa neema kodi majengo, madini
Mbunge awatwisha zigo Chadema, 'Hawa ni wanahusika wakuu'