Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola amesema kuwa vitambulisho vya taifa vitatolewa kwa Watanzania wenye sifa ambao watapita katika mchujo ili kuepusha kutoa kwa wahamiaji haramu.

Amesema kuwa mchujo huo unaofanywa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) upo makini ili kuhakikisha hakuna makosa yatakayofanywa wakati wa utoaji wa vitambulisho, hivyo wananchi wawe na uvumilivu wakati mchujo huo ukiendelea.

Lugola ameyasema hayo wakati alipokua anazungumza wananchi wa jimbo lake katika Kijiji cha Mwisenyi, Kata ya Butimba, Wilayani Bunda Mkoa wa Mara na kuwataka wapiga kura wake na Watanzania kwa ujumla wawe na subira wakati hatua za utambuzi na usajili zikiendelea kufanyika sehemu mbalimbali nchini.

“Hakuna Mtanzania mwenye sifa atakayekosa kitambulisho cha taifa, lakini lazima muwe na subira wakati zoezi la utambuzi wa watu gani wanaweza kupata vitambulisho hivi, na pia katika utambuzi tunapaswa kuwa makini sana kwasababu tusije tukapenyeza wahamiaji haramu wasiostahili na wao wakaweza kupata vitambulisho na baadaye tukaja kupata shida,” amesema Lugola.

Aidha, amesema kuwa baada ya hatua ya utambuzi, inafuata hatua ya usajili ambayo pia hatua hiyo nayo inahitaji umakini mkubwa zaidi na ikimalizika hatua hiyo majina yaliyosajiliwa yanarudishwa tena kwa wananchi kuulizwa kama waliosajiliwa wanatambuliwa katika sehemu wanazoishi, hatua hiyo ikiwa na lengo la kupata taarifa sahihi ya waliosajiliwa wanatambuliwa au hawatambuliwi na wazawa katika eneo.

Hata hivyo, Lugola ametoa shilingi milioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati ambao ulisimama kwa zaidi ya miaka sita kutokana na ukosefu wa fedha, na pia ameendesha harambee kwa madiwani na maafisa alioambatana nao katika mkutano huo, na kufanikiwa kuchangisha shilingi milioni moja na elfu ishirini.

 

Ziwa Victoria lazidi kuwa hatari, wengine 14 wafa maji
Serikali CCM haihitaji mabaidiliko- Shaka