Hatimaye watoto 12 wa kiume wa timu ya soka nchini Thailand pamoja na kocha wao waliokuwa wamenasa kwenye pango kwa siku tisa, wameokolewa.

Mkuu wa kitengo cha maji wa Jeshi la Thailand amesema kuwa hatimaye ndoto ya kuwapata watoto wote na kocha wao wakiwa hai kutoka kwenye mapango ya Tham Luang imekuwa kweli.

Watoto hao wenye umri wa kati ya miaka 13 na 17, wakiwa na kocha wao walitoweka tangu Juni 23.

“Tulikuwa na matumaini kuwa wanaweza kuwa hai lakini tulipaswa kufanya jitihada, tulitakiwa kwenda mbele,” Rear Adm Arpakorn Yuukongkaew anakaririwa na BBC.

Aliongeza kuwa kulikuwa na punje ya matumaini ya kuwapata wakiwa hai kutokana na hali halisi ya mazingira pamoja na kukosa chakula kwa siku tisa lakini wanamshukuru Mungu wamekutwa wakiwa salama.

Tukio la kunasa kwa watoto hao pamoja na kocha wao lililoiteka mijadala ya vyombo vya habari duniani na maombi kuelekezwa kwao, lilitokea baada ya timu hiyo kwenda kwenye mapango hayo baada ya kufanya mazoezi lakini maji mengi yaliyofurika kwenye njia walizopita yalisababisha kushindwa kutoka.

Kupitia timu ya waokoaji wabobezi kutoka nchi mbalimbali, zoezi la siku tatu lilisababisha watoto wanne Jumapili iliyopita, watoto wengine wanne Jumatatu, na hatimaye jana watoto wanne waliosalia pamoja na kocha wao.

Maafisa wa Thailand wameeleza kuwa baada ya kufanya mahojiano na timu hiyo kufahamu jinsi walivyoweza kuishi ndani ya pango hilo, waliwaeleza kuwa waliishi kwa kunywa maji yaliyokuwa yanapita kwenye maporomoko ya mapango hayo.

Watoto wote 12 na kocha wao wamefikishwa kwenye hospitali ya jiji la Chiang Rai na wanaendelea kupatiwa matibabu ikiwa ni pamoja na matibabu ya kisaikolojia, kwa mujibu wa taarifa ya Serikali.

 

Riyad Mahrez aahidi mazito Man City
Nauli za ndege mpya Boeing 787-8 Dreamliner hizi hapa, sawa na bure