Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Zaituni Bokhari amesema baada ya vipimo imegundulika kuna uwezekano mkubwa wa kuwatenganisha watoto pacha walioungana.

Dk Bokhari ambaye amebobea katika upasuaji huo Afrika Mashariki, ameyasema hayo leo asubuhi alipokuwa akitoa majibu ya vipimo vilivyochukuliwa hospitalini hapo kwa takribani wiki nzima.

“Vipimo vya damu vimeonyesha kila mtoto ana mfumo wake na hawana maambukizi ya aina yoyote, ugumu unakuja kwenye ini na moyo ambapo wanategemeana ila uwezekano wa kutenganishwa upo,”amesema Dk Bokhari.

Majibu hayo yamekuja siku chache baada ya pacha hao kupimwa vipimo vya radiolojia ikiwemo CT Scan, MRI, X Ray kipimo cha moyo (ECO) pamoja na vipimo vyote vya damu.

Watoto hao waliozaliwa katika hospitali ya Misheni ya Berega iliyopo Kanda ya Mashariki mkoani Morogoro, Julai 21 mwaka huu wameaza kuchukuliwa vipimo mbalimbali vya awali.

Wakimbizi raia wa Burundi waitikia wito wa JPM
Video: CCM inalinga tu kwa sababu inabebwa na dola-Sumaye