Wafanyabiashara wa Pembejeo mikoa ya kusini wametakiwa kufanya biashara kwa kufuata utaratibu na miongozo ya serikali ili kuepukana na madhara ya adhabu ya kifungo au faini zitakazotolewa pindi mfanyabiashara atakapobainika anafanya biashara kinyume na utaratibu.

Hayo yamesemwa wilayani Njombe na mtaalamu kutoka shirika la TAPBDS, Deodant Bernad katika mradi wa AGRA TIJA Tanzania unaofanya kazi katika mikoa mitatu ya Iringa, Njombe na Ruvuma katika sekta ya kilimo.

Amesema kuwa miongoni mwa utaratibu wanaotakiwa kuwa nao wafanyabiashara ni pamoja na kuwa na vibali vya TPRI kwa ajili ya kuuza na kutoa huduma vya viwatilifu vizuri na kwa usahihi, kuwa na vibali vya uuzaji wa mbolea TFRA pamoja na kibali cha uuzaji wa mbegu kutoka TOSC huku wakifuata umuhimu wa utunzaji wa kumbukumbu wa biashara zao.

“Kama tulivyoelekezwa kuwa sheria zote kuanzia TOSC, TPRI na TFRA wakaguzi wa mbolea wapo na wanafanya kazi na wameongezewa nguvu na serikali ya awamu hii, kwa hiyo endapo atakutwa mtu anafanya kazi kinyume na utaratibu kuna faini, kifungo au vyote kwa pamoja na haya ni madhara ya moja kwa moja lakini pia yapo madhara yasiyoonekana kwa haraka hususani kwa mkulima endapo msambazaji wa pembejeo akafungiwa biashara yake,”amesema Bernad

Kwa upande wake Afisa kilimo wa mkoa wa Njombe Wilson Joel amesema kuwa wadau wa kilimo wamekuwa na msaada mkubwa katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara, maafisa ugani na wakulima ili kuwasaidia hususani katika vipindi vya kilimo.

Nao baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria mafunzo hayo wamesema kuwa elimu hiyo itasaidia zaidi kutoa maelekezo kwa wakulima namna ya matumizi bora ya pembejeo na kuahidi kufuata utaratibu wa serikali.

 

Breaking news: Ephraim Kibonde wa Clouds FM amefariki dunia
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Machi 7, 2019