Mtu yeyote atakaye ruhusu mtoto chini ya miaka 18 kushiriki, kuingia au kukaa karibu na eneo la mchezo wa kubahatisha (kamari) anahesabiwa kufanya kosa.

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji, Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge Viti Maalum Asha Abdullah Juma juu ya kuongezeka kwa maduka ya kucheza Kamari yanayojulikana kama Jack Pot katika miji mingi hapa nchini hivyo kusababisha uvunjifu wa maadili na nguvu kazi ya vijana.

“Michezo yote ya kubahatisha ikiwemo kamari (slots machines) inaendeshwa kwa mujibu wa sheria ya Bodi ya Michezo ya kubahatisha namba 4 ya mwaka 2003, sura 41 pamoja na Kanuni zake,” amesema Dkt. Kijaji.

Amesema kuwa, kwa mujibu wa sheria hiyo hakuna mtu au taasisi inayoruhusiwa kuendesha biashara ya michezo ya kubahatisha bila kuwa na leseni kutoka Bodi ya Michezo ya kubahatisha pamoja na vibali vingine vinavyotolewa na mamlaka nyingine za biashara.

Vile vile sheria hiyo inakataza watoto wenye umri chini ya miaka 18 kushiriki, kuingia, kukaa au kuzururazurura karibu na maeneo ya michezo ya kubahatisha.

Aidha ameongeza kuwa mtu yeyote ambaye atamruhusu mtoto chini ya miaka 18, kushiriki, kuingia au kukaa karibu na eneo la mchezo wa kubahatisha anahesabika kufanya kosa na anastahili kulipa faini ya shilingi 500,000 au kifungo kisichopungua miezi mitatu au vyote kwa pamoja.

Hata hivyo amesema kuwa, michezo hiyo inaendeshwa kwa mujibu na sheria kama shughuli nyingine. Jambo la msingi ni kuhakikisha kuwa, wanaoendesha michezo hiyo wanazingatia sheria na kanuni zilizowekwa pamoja na wazazi, walezi na jamii kuhakikisha vijana wanazingatia mila na desturi zinazolinda maadili ya Kitanzania wanapokuwa wanajishughulisha na shughuli halali za kiuchumi.

#HapoKale
Kwesigabo: Mfumuko wa bei unakua kwa kasi ndogo