Halmashauri ya wilaya ya Magu mkoani Mwanza imefanikiwa kuwakabidhi wazee 25499 vitambulisho kwa ajili ya kupata matibabu bure.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Dkt. Philemon Sengati wakati akikabidhi vitambulisho hivyo kwa wazee hao, ambapo amesema kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli imejipanga kuhakikisha wazee wote nchini wanapata matibabu bila malipo kama walivyoahidiwa mwaka 2015 wakati wa kampeni.

Amesema kuwa mbali na kuwakabidhi vitambulisho wazee hao, pia limetengwa dirisha maalum kwa ajili ya utoaji wa huduma kwa wazee ili kurahisisha kufikia huduma bila kupanga foleni kutokana na umri wao.

Naye mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Lutengano Mwaliba ameipongeza Idara ya Ustawi wa Jamii kwa utekelezaji wa ahadi ya serikali kwa kuwapatia wazee vitambulisho vya huduma za kiafya na kuwataka wazee wote waliotimiza miaka 60 kufika ofisini kwake ili waweze kuandikishwa na kupatiwa vitambulisho kwa ajili ya matibabu.

Kwa upande wao wazee wameipongeza serikali ya awamu ya tano kwa kutekeleza ahadi ya kutoa matibabu bure kwa wazee huku wakiiomba serikali kuendelea kuwasimamia watoaji wa huduma za afya kwani wengi wao wamekuwa na tabia za kuwaona wazee kama si watu huku kila mtu ni mzee mtarajiwa.

Aweso atumbua mkandarasi wa maji mkoani Kagera
Mwanamke ajitolea kulea sokwe yatima