Wazee, Walemavu, Wajane na Watu wasiojiweza katika vijiji vinavyopakana na hifadhi ya Taifa Serengeti SENAPA wamenufaika na hati miliki za kimila jambo ambalo litasaidia kupunguza Migogoro ya Ardhi katika Wilaya ya Tarime Mkoani Mara.

Akisoma taarifa kwa kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru kitaifa, Mkongea Ali, Mkuu wa idara ya Ardhi na Maliasili, Rhoida Nyondo amesema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kwa kushirikiana na tume ya Taifa ya mipango ya matumizi ya bora ya Ardhi wanaendelea na uandaaji wa mipango bora ya matumizi ya ardhi katika vijiji 16 vinavyopakana na hifadhi ya Taifa Serengeti pamoja na bonde la Mto Mara kwenye hifadhi ya Mbuga ya Taifa Serengeti ili kupunguza Migogoro.


“Zoezi la  uandaaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi  linaenda sambamba na urasimishaji  wa ardhi vijijini na kutoa hati ya haki miliki za kimila kwa wananchi 25 kutoka kwenye makundi maalumu, walemavu, wajane, na wazee sawa na hati miliki 400 katika vijiji 16 vinavyonufaika na mradi huo,” amesema Rhoida.


Amesema kuwa uwepo wa hati miliki utasaidia kupunguza utumiaji wa matumizi ya ardhi kiholela huku wakitumia hati miliki hizo kukopa kwa ajili ya kujiongezea kipato.


Kwa upande wake Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Massana Mwishawa amesema kuwa wao wamegharamia upatikanaji wa hati hizo na kudai kuwa zoezi litafanyika nchi nzima kwa lengo la kupunguza Migogoro baina ya hifadhi na vijiji vinavyowazunguka.

 

Nao baadhi ya wazee wawakilishi ambao wamepatiwa hati hizo katika mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2019 katikja Viwanja vya Ingwe Sekondari wanatoa shukrani kwa serikali kwa kutambua makundi maalumu bila kusahau wajane.

RC Hapi awashangaa waandishi wa habari, 'Msirudie tena'
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Juni 6, 2019