Wajumbe wa Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Nchini (TACIP) wamemtembelea Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe ofisini kwake jijini Dar es salaam ili kumpa taarifa za maendeleo ya mradi huo ambao upo chini ya Wizara yake.

Wajumbe hao ni Kaimu Katibu Mtendaji toka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Onesmo Kayanda, Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA), Adrian Nyangamalle, Mkurugenzi wa Biashara na Uhusiano toka DataVision International, Teddy Qirtu na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasilano (TEHAMA) kutoka DataVision International, Dkt. Dkt. Shaban Kiwanga.

Waziri Mwakyembe amefurahishwa sana na maendeleo ya mradi huo kwani pamoja na changamoto mbali mbali zilizolipotiwa na wajumbe hao, lakini bado hawajakata tamaa wala kurudi nyuma bali wameendelea kusonga mbele kuhakikisha mradi huo wenye lengo kubwa la kuwainua wasanii wa sanaa za ufundi nchini unafanikiwa kwa kiasi kikubwa kama ambavyo umekusudiwa.

Awali akizungumza Rais wa TACFA, Andrian Nyangamalle, amesema kuwa tangu mradi huo ufunguliwe rasmi umeweza kufanya mambo mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa unawafikia wasanii hao katika maeneo yao, ili kuwasajili, kutoa semina mbali mbali, na kutoa fursa kwa wasanii kutangaza na kuuza kazi zao katika matamasha na maonyesho mbali mbali.

Pamoja na hayo, Adrian amemweleza Waziri Mwakyembe kuwa wameendelea kuutangaza mradi huo, ambapo hadi sasa hivi wameutambulisha na kukubalika kwa kiasi kikubwa sana  kwa Mkoa wa Dar es salaam, kupitia Mkuun wa Mkoa huo, Paul Makonda, Mkoa wa Arusha kupitia mkuu wa mkoa huo, Mrisho Gambo na Mkoa wa Morogoro kupitia kwa mkuu wa mkoa huo, Dkt. Steven Kebwe.

Amesema kuwa ili kuwafikia wasanii wameendesha zoezi la Mtaa kwa Mtaa ili kuwafikia wasanii popote walipo ambapo tayari zoezi hilo limeendeshwa katika Wilaya ya Kinondoni na kuweshesha wasanii zaidi ya 6,000 kuandikishwa katika mradi huo.

Naye, Mkurugenzi wa Biashara na Uhusiano toka DataVision International, Teddy Qirtu amesema kuwa kampuni hiyo imeendelea kuboresha na kuwekeza katika teknolojia na ina zaidi ya miaka 20 katika utendaji hivyo ubunifu wao katika mfumo wa kisasa wa TACIP umeanza kuzaa matunda kwa kuwawezesha wasanii kutambulika, kuanza kukopesheka na kuneemeka baada ya kujiunga na mradi huo.

Kufuatia taarifa hizo katika hatua ya utekelezaji mradi huo, Waziri Mwakyembe amepongeza juhudi hizo za utekelezaji mradi huo, na ameahidi ushirikiano na kwenda sambamba zaidi ili kuhakikisha mradi huo unafikia malengo yake.

Amesema changamoto zote zinatekelezeka na yeye kwa nafasi yake atahakikisha anazitatua, kwani mradi huo ni neema kubwa kwa wasanii na Taifa kwa ujumla.

Aidha, Waziri Mwakyembe ameipongeza Kampuni ya DataVision International kwa juhudi kubwa inayofanywa na Kampuni hiyo katika masuala ya Teknolojia nchini.

Amesema kuwa, kupitia teknolojia ya DataVision katika mradi huo wasanii wataweza kupata thamani ya jasho lao wanalovuja juu ya kazi hizo.

Hivyo, ameitaka kampuni hiyo kujitokeza katika tenda mbali mbali zinazotangazwa na Serikali ya Rais Magufuli kwani wanavigezo vyote na hawana mshindani kutokana na kazi kubwa wanazofanya kwa ubora mkubwa tena wakitanguliza mbele uzalendo kwa Taifa lao.

“DataVision ni kampuni ya kizalendo sana, juhudi zenu zinaonekana, jinsi mnavyotumia teknolojia na kuvumbua miradi mbali mbali yenye lengo la kuwakomboa watanzania, nawaomba sana DataVision msichoke, jitokezeni katika tenda za Serikali kwani kazi yenu ni bora sana.” Amesema Waziri Mwakyembe.

TACIP ni mradi wa utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania ambao umevumbuliwa na kampuni ya kizawa ya DataVision International iliyoko jijini Dar es Salaam, inayojishughulisha na masuala ya Teknlolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Tafiti na Mafunzo, ambapo wanatekeleza mradi huo kwa kushirikiana na Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA) chini ya Wizara ya Habari, Sanaa na Michezo. Mlezi wa mradi huo ni Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda.

 

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akizungumza na wadau wa Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP) wakati walipomtembelea ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya mradi huo.

Kaimu Katibu Mtendaji toka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Onesmo Kayanda (kushoto) akifafanua jambo kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe wakati wadau wa Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP) walipomtembelea Waziri Mwakyembe katika ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya mradi huo.

Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA) Adrian Nyangamalle (kulia) akifafanua jambo kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe wakati walipomtembelea ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP).

Mkurugenzi wa Biashara na Uhusiano toka DataVision International, Teddy Qirtu (kulia) akifafanua jambo kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (kushoto) wakati walipomtembelea ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP), katikati ni Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA) Bw. Adrian Nyangamalle.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akiangalia kadi ya utambuzi wa wasanii wa sanaa za ufundi wakati alipotembelewa na wadau wa Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP) katika ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya mradi huo.

Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasilano (TEHAMA) toka DataVision International, Dkt. Dkt. Shaban Kiwanga ( kulia) akifafanua jambo kwa  Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (kushoto) wakati walipomtembelea ofisi ndogo za Dar es Salaam kwa lengo la kutoa tathmini ya maendeleo ya Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi Tanzania (TACIP),  wa pili toka kushoto ni Rais wa Shirikisho la Sanaa za Ufundi Tanzania (TAFCA) na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Biashara na Uhusiano toka DataVision International, Teddy Qirtu.

Tabia hizi ni hatari kwa Ubongo wako
Ahadi zote alizoahidi JPM zitatekelezwa- Majaliwa