Yamebaki masaa machache kushuhudia taifa la Tanzania likiweka historia nyingine itakapovaana na Lesotho jioni ya leo, historia ambayo haitofutika milele endapo timu ya taifa Taifa Stars itapata alama tatu zitakazoipeleka michuano ya AFCON nchini Cameroon mwakani.

Taifa Stars iliyopo katika kundi L, inashika nafasi ya pili kwa alama 5 nyuma ya kinara Uganda yenye alama 13 baada ya kushinda mchezo wa jana na kujikatia tiketi ya kufuzu michuano hiyo. Nafasi ya tatu ikishikiliwa na Cape Verde yenye alama 4 na Lesotho ikiburuza mkia kwa alama 2.

Aidha, Stars inahitaji kushinda mchezo wa leo ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu AFCON mwakani, ambapo itafikisha jumla ya alama 8 ambazo hata ikipoteza mchezo wake wa mwisho dhidi ya Uganda haitoweza kufikiwa na Cape Verde ambayo itakuwa na alama 7 endapo itashinda mchezo wake wa mwisho dhidi ya Lesotho.

Akizungumza kuelekea mchezo huo, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe ameitaka Taifa Stars kutowaangusha Watanzania zaidi ya milioni 50 ambao leo wako nyuma yao katika mchezo huo.

“Ile hali tuliyoionyesha wakati tunacheza na Cape Verde nyumbani tuionyeshe sasa, tena iwe mara mbili, Watanzania zaidi ya milioni 50 wako nyuma yenu wanawaangalia. Nawaomba sana!! sana!! tena sana!! Taifa Stars tusimuangushe Rais Magufuli,” amesema Mwakyembe

Ikumbukwe kuwa Taifa Stars imeshiriki mara moja pekee katika michuano ya mataifa ya Afrika, ambayo ni mwaka 1980 nchini Nigeria. Nafasi ya mwaka huu ni nafasi pekee ambayo itaweka historia kwa mara ya pili kushiriki michuano hiyo baada ya takribani miaka 38

Taifa Stars yapoteza alama 3 Lesotho
Benki ya Dunia yaelezea sharti la mkopo wa elimu Tanzania