Shirika la Afya Duniani, WHO, limesema kuwa limechukua hatua za haraka kukabiliana na mlipuko wa virusi vya Ebola nchini Uganda, huku hatua madhubuti zikichukuliwa kuhakikisha kwamba watu wanaoishi kwenye mpaka wa Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wanaanza kupokea chanjo dhidi ya Ebola.

Taarifa iliyotolewa na msemaji wa shirika la afya duniani WHO nchini Uganda, Irene Nakasiita imesema kuwa wataalam wa kupambana na Ebola wametumwa katika wilaya ya Kasese, mpakani na Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kuweka mikakati ya dharura kuzuia virusi vya ebola kusambaa kwa umma.

Hii ni baada ya mtoto mvulana mwenye umri wa miaka mitano kuaga dunia, siku moja baada ya familia yake kutembelea watu wa ukoo wake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Aidha, shirika la afya duniani limesema ripoti za Ebola nchini Uganda ni za kutisha, lakini kwa ushirikiano na wizara ya afya ya Uganda, wamekuwa wakiweka mikakati ya kujitayarisha dhidi ya ugonjwa huo.

Kwa upande wake waziri wa afya wa Uganda, Jane Ruth Aceng amesema kuwa chanjo dhidi ya ebola katika wilaya ya Kasese na sehemu zilizo karibu, itaanza kutolewa ijumaa ya wiki hii.

“Wizara ya afya, shirika la afya duniani na kituo cha kukabiliana na magonjwa ya kuambukiza, wataanza kutoa chanjo dhidi ya Ebola kwa watu wanaoaminika kuwa karibu na maeneo  yaliyothibitishwa kabla ya chanjo kutolewa kwa uma, kuanzia juni 14.”amesema Aceng

Hata hivyo, watu wanane wa familia ya mtoto aliyeaga dunia wakiwemo wazazi wake, na jamii waliyoitembelea DRC, wanachunguzwa na bibi ya marehemu mwenye umri wa miaka 50 wamethibitishwa kuambukizwa.

 

Miley Cyrus aomba radhi kwa kuiponda Hip-Hop
LIVE IKULU: Rais Dkt. Magufuli akutana na Wabunifu wadogo wa kufua umeme