Mwanamke mmoja aliyetambulika kwa jina la Cecilia Paschal mkazi wa Kisimani wilayani Simanjiro Mkoani Manyara anadaiwa kumuua mtoto wake mdogo mwenye umri wa miezi sita baada ya kuibuka ugomvi kati yake na mumewe uliosababishwa na wivu wa mapenzi.

Inadaiwa kuwa Cecilia alitekeleza tukio hilo la kumchinja mwanaye kwa kisu na kitu kinachodhaniwa kuwa ni kisu, kisha kutaka kujiua mwenyewe kwa kumeza dawa za aina mbalimbali.

Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa polisi Mkoa wa manyara, Augustino Senga alipozungumza na waandishi wa habari amesema kuwa tukio hilo lilitokea Januari 20, majira ya saa 12 jioni.

“Chanzo cha tukio hili ni wivu wa kimapenzi kwa sababu kabla ya tukio, inaelezwa alikuta namba ya simu ya mwanamke katika simu ya mumewe, baada ya kuona namba ya simu ya mwanamke huyo ikitumika kuwasiliana na mumewe kila wakati, Januari 19, ndipo ukatokea ugomvi kati yao,’ alisema Kamanda Senga.

Kwa mujibu wa Kamanda Senga, mume wa Cecilia aliamua kuondoka nyumbani mpaka alipojulishwa madai ya mwanaye kuchinjwa ndipo akarejea nyumbani. Alisema ameongeza kuwa Mwili wa mtoto huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya wilaya ya Hai kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi.

Baada ya jaribio la kujiua kwa dawa mbalimbali kushindikana, mtuhumiwa alipelekwa kituo cha Afya Mererani, ambako anapatiwa matibabu chini ya ulinzi wa polisi na atapelekwa mahakamani baada ya upelelezi wa awali kukamilika.

Kamanda Senga amemalizia kuwa kitendo kinachodaiwa kufanywa na mwanamke huyo ni cha kikatili, na ametoa wito kwa wananchi kuepuka kuvunja sheria kwa vigezo vya hasira na wivu.

 

 

Video: UVCCM, UDSM yafafanua faida za Ndege Mpya
Video: Mahojiano ya Lissu, BBC yalivyotikisa dunia haya hapa