Madudu mengine yameibuliwa katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia baada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serilali (PAC) kupitia taarifa za Manunuzi na za kihasibu za wizara hiyo wakati sakata la wanafunzi hewa likiendelea kufukuta.

Kamati hiyo imebaini kuwa shilingi bilioni 1.2 zilitumika kwa ajili ya kuandaa hafla ya harambee ya Wizara hiyo nchini Marekani, tukio ambalo hata hivyo halikufanyika.

Kwa mujibu wa maelezo ya wizara hiyo, harambee hiyo ilitarajiwa kukusanya zaidi ya dola milioni 3 za Marekani ambazo ni sawa na shilingi bilioni 6 za Kitanzania.

Wajumbe wa PAC walihoji matumizi ya fedha hizo. Hivyo, Gerald Mwaja ambaye anahusika na mipango alilazimika kutoa majibu ambayo hata hivyo yalionekana kutowaridhisha wajumbe wa Kamati hiyo.

Alisema kuwa fedha hizo zilitumika kwa ajili ya mradi huo ambao ulikuwa na malengo matatu, kati ya malengo hayo lengo moja la kufanya harambee hiyo lilishindwa lakini malengo mengine mawili yalifanikiwa.

“Mradi wenyewe ulikuwa na malengo matatu; kuongeza matumizi ya teknolojia ya Mawasiliano, kuja na mbinu za kufundishia na pia kukusanya fedha kwa awamu,” alisema.

Alisema malengo mawili yaliyotimia ni kuongeza matumizi ya teknolojia ya mawasiliano pamoja na mbinu ya kufundishia.

Katika hatua nyingine, PAC imebaini kuwa Wizara hiyo ilitenga kiasi cha shilingi bilioni 2.1 na kuingia mkataba na Kampuni ya Ujenzi ya Magereza mwaka 2014 kwa ajili ya kujenga jengo la ghorofa tatu la ofisi za wizara hiyo Mkoani Dodoma lakini jengo hilo halijajengwa hadi sasa.

Mbunge wa VWawa (CCM), Josephat Asunga alisema kuwa wamebaini kuwa sheria ya manunuzi ya umma haikufuatwa na kwamba mkandarasi alilipwa kiasi shilingi milioni 780.6 kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo hata kabla ya mkataba kusainiwa.

Aliongeza kuwa hakukuwa na maelezo yoyote yanayoonesha kulikuwa na mshindani katika zabuni hiyo huku fedha nazo zikilipwa kwenye akaunti ya mtu aliyetajwa kwa jina la Mang’ula badala ya akaunti ya kampuni ya Magereza.

Pia, Asunga alieleza kuwa kabla ya ujenzi kuanza mwaka 2015, Wizara hiyo ilibadili mpango wa kujenga jengo hilo kwa ghorofa tatu na kuwa jengo la ghorofa nne litakalogharimu shilingi bilioni 4.4.

“Baada ya Rais Magufuli kuagiza kuwa wote tunahamia Dodoma, wamebadilika wanasema hawajapata eneo la ujenzi wakati walishasema awali wamepata eneo,” alisema Asunga.

Dk. Makame Mbarawa ambaye alikuwa Waziri wa Elimu wakati huo, alieleza kuwa hakufahamishwa lolote kuhusu ujenzi wa jengo hilo na kwamba hata muhtasari wa mpango huo hakupewa kwa ajili ya kushauri.

“Mimi kama Waziri sikujua kinachoendelea katika ujenzi wa jengo, na hata briefing (muhtasari) ilikosekana ili niweze kushauri,” alisema.

Akijibu maswali hayo, Afisa Manunuzi wa Wizara hiyo, Audifasy Myonga alikiri kuwa utaratibu wa manunuzi haukufuatwa na kwamba kulipaswa kuwa na mshauri mwelekezi ili kutimiza matakwa ya Sheria.

Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Hillary Aeshi aliagiza kupitiwa upya kwa mchakato wa zabuni ya Jengo la ofisi ya wizara hiyo mjini Dodoma na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji kwenye ofisi ya Katibu wa Bunge kabla ya Septemba Mosi mwaka huu.

Ndanda FC Washindwa Kufurukuta, Wakubali Kufungwa 3-1
Mfanyabiashara ajiua kwa kujilipua na Petroli