Jeshi la Polisi Mkoani Morogoro linawashikilia watu watatu ambao ni vinara wa matukio ya utapeli pamoja na wizi kwa njia ya mtandao wakiwa na simu 9 pamoja na line 57 za mitandao mbalimbali zinazotumika kufanya utapeli.

Watuhumiwa hao wamekuwa wakiiba kwa kutumia mbinu ya kuchukua namba za makamanda mbalimbali zilizowekwa katika mitandao kwa ajili ya kusaidia wananchi pindi yatokeapo matukio ya uhalifu au kupata ufafanuzi juu ya matukio mbalimbali yanayotokea katika eneo fulani.

Hivyo kupitia namba hizo wamekuwa wakizitumia kwa kujipatia fedha kwa kuwapigia watu mbalimbali na kuomba kiasi fulani cha pesa huku wakidai kuwa yeye ni kamanda fulani yupo kwenye kikao hivyo anaomba msaada wa haraka wa kifedha.

Kamanda Matei ameeleza wamekuwa wakitumia namba hizo kuwaibia watu mbalimbali kwa kutumia kivuli cha cha majina ya makanda hao wa polisi, na watu wamekuwa wakiwatumia fedha hizo wakidhani kuwa wamemtumia kamanda kutokana na zile namba zao.

Hayo yamethibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei na kusema tayari watuhumiwa hao wapo chini ya ulinzi wa polisi mkoani humo.

Aidha jeshi la polisi kwa kushirikiana na timu ya wataalam wa makosa ya mitandao pamoja na Kikosi cha kupambana na ujambazi wamefanikisha kupatikana kwa majambazi hao na wanawashikilia kwa maelezo zaidi kuhusu mbinu wanazozitumia ili kusaidia kudhibiti matukio hayo na mengine kama hayo.

Ureno yachezea kichapo kutoka Uholanzi
Walawiti 6 washikiliwa na polisi