Baada ya hivi karibuni Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutangaza kuzihamishia mechi za Simba na Yanga katika Uwanja wa Uhuru baada ya kukamilika kwa ukarabati wake, mapya yameibuka kuhusiana na uwanja huo.

Daktari wa Yanga, Edward Bavo, ameonyesha wasiwasi wake kuwa timu hiyo inaweza kukumbwa na majeraha ya wachezaji wengi pindi itakapoanza kuutumia uwanja huo kutokana na sehemu ya kuchezea kuwa ngumu ukilinganisha na Uwanja wa Taifa.

Kutokana na hali hiyo, Bavo alisema kuwa inabidi uongozi wa Yanga uwatafutie wachezaji wake hao viatu maalum ambavyo watakuwa wakivitumia katika uwanja huo ili kuendana na hali halisi.

“Uamuzi huo wa serikali siyo mbaya lakini uwanja huo haukupaswa kutumika hivi sasa mpaka hapo sehemu ya kuchezea itakapofanyiwa marekebisho kwani ni ngumu sana, vinginevyo wachezaji wengi watakumbwa na majeraha.

“Ile siku moja tu tuliyofanya mazoezi katika uwanja huo tulipokuwa tunajiandaa na safari yetu ya kuja Congo (DR Congo), kucheza na TP Mazembe, wachezaji wetu wawili waliumia, hiyo ilikuwa mazoezini tu, vipi kwenye mechi,” alihoji Bavo kisha akaongeza:

“Kutokana na hali hiyo, inabidi sasa uongozi wetu uangalie uwezekano wa kuwanunulia viatu maalum wachezaji watakavyokuwa wakivitumia katika uwanja huo ili kujilinda na majeraha wanayoweza kuyapata na kutuvurugia mipango yetu ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu kwa mara nyingine tena,” alisema.

Yanga itaanza kuutumia uwanja huo Jumapili ijayo itakapopambana na African Lyon katika mchezo wake wa kwanza wa ligi.

Chanzo: Gazeti La Championi

Mwanariadha Wa Ethiopia Asaidiwa
Mr Blue amfananisha Baraka Da Prince na Bajaji, “hawezi kugongana na Meli”