Mchezo wa Robo Fainali ya Nne ya Kombe la Shirikisho la Azam (Azam Sports Federation Cup 2016/2017), kati ya Young Africans na Tanzania Prisons FC utafanyika kesho Aprili 22, 2017 saa 10.00 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Mchezo huo utatoa mshindi ambaye ataungana na timu nyingine tatu ambazo tayari zimefuzu kwa hatua ya Nusu Fainali. Timu zilizotangulia Nusu Fainali ya ASFC ni za Mbao FC, Simba SC na Azam FC.

Jumapili Aprili 23, mwaka huu kutakuwa na droo ya wazi kwa timu nne zitakazokuwa zimefuzu kwa hatua ya Nusu Fainali ya ASFC, itakayofanyika Kituo cha Televisheni cha Azam ambao ni wadhamini wakuu wa jina la michuano na haki ya kuonesha mubashara michuano hii ambayo inafanyika kwa msimu wa pili mfululizo.

Azam FC ilikata tiketi ya kucheza Nusu Fainali ya ASFC baada ya kuifunga Ndanda FC mabao 3-1, kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam Aprili 5, 2017 ikitanguliwa na Mbao iliyoishinda Kagera Sugar mabao 2-1 katika mchezo ulifanyika Uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera Machi 18, 2017 ilihali Machi 19, mwaka huu Simba iliwatoa Madini ya Arusha kwenye mchezo uliofanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.

Nusu Fainali inatarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu, kabla ya fainali ambako Bingwa wa michuano hii ambayo msimu huu ilishirikisha timu 86 ikiwa ni pamoja na za Ligi Kuu ya Vodacom (timu 16); Ligi Daraja la Kwanza (timu 24); Ligi Daraja la Pili (timu 24) na mabingwa wa mikoa timu 22, atazawadiwa Sh. 50 milioni na kupata tiketi ya kuiwakilisha nchi katika michuano ya Kombe la Shirikisho – CAF.

Video: Majaliwa ataka watanzania kuwa kitu kimoja
UEFA Wamaliza Ubishi Wa Nusu Fainali