Kiungo mshambuliaji mpya wa Mbeya City fc , Zahor Pazzy amemshukuru rais wa shirikisho la kabumbu nchini Jamal Malinzi kwa kufanikisha kupatikana kwa hati yake ya uhamisho (ITC) iliyokuwa imekwama nchini DR Congo kwa miaka miwili.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa mazoezi ya leo kwenye uwanja wa Sokoine jijini hapa, Zahor amesema kuwa anafuraha kubwa kuona amerudi rasmi kwenye ulimwengu wa soka baada ya kukaa nje kwa miaka miwili, licha ya jitihada kubwa alizokuwa akizifanya.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu, hakika natanguliza sifa kwake, nimekuwa nje ya soka la ushindani kwa miaka miwili sasa, mara kadhaa nimejaribu kufanya jitihada za kuhakikisha naokoa kipaji changu lakini sikufanikiwa,” alisema.
“Namshukuru rais wa TFF amefanikisha ndoto zangu za kuendelea kucheza mpira. Niseme wazi kuna wakati nilikata tamaa kabisa, ingawa pia niliendelea kujipa moyo na kumuomba Mungu, nashukuru sasa niko huru na naweza kuitumikia timu yangu mpya,” aliongeza.
Mchezaji huyo pia aliwashukuru viongozi wa Mbeya City Fc kwa kumpa nafasi ya kuitumikia timu hiyo licha ya kutokuwa kwenye soka la ushindani kwa muda mrefu. Alisema kuwa anaamini kwa jitihada za wachezaji na uongozi wa timu hiyo, wataibuka na ushindi dhidi ya Mbao FC, Jumamosi hii.
Alitoa wito kwa wachezaji wenzake kuwa makini katika masuala ya usajili na uhamisho ili wasikutwe na majanga yaliyomkwamisha kwa miaka miwili.