Serikali nchini, imetumia kiasi cha shilingi milioni 710.7 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya utalii ya Pori la Akiba Pande ili kuhakikisha kuwa pori hilo linaendelea kuwa kitovu cha utalii jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja ameyasema hayo Bungeni jijini Dodoma kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, wakati akijibu swali la Mbunge wa Kibamba, Issa Mtemvu aliyetaka kujua mikakati ya Serikali ya kutumia Pori la Akiba Mabwepande kama chanzo cha mapato.

Amesema, fedha hizo zimetumika katika ujenzi wa Kambi za Watalii mbili katika eneo la Msakuzi na Jomeke na ujenzi wa maeneo mawili kwa ajili ya watalii kupumzika na kupata huduma mbalimbali, katika eneo la Bwawani na Crater pamoja na ujenzi wa uzio wa bustani ya wanyamapori kwa lengo la kukuza utalii katika eneo hilo.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja.

“Ujenzi wa miradi ya miundombinu hiyo umekamilika na imeanza kutumiwa na watalii ambapo kwa sasa shughuli mbalimbali zikiwemo mbio za Marathon, nyama choma Festival, utalii wa kutembea kwa miguu na kuendesha baiskeli, upigaji picha na matamasha mbalimbali yamekuwa yakifanyika” Amefafanua Masanja.

Akijibu swali la Mbunge wa Lupa, Masache Kasaka kuhusu Serikali kupunguza eneo la Msitu wa Mbiwe uliopo Chunya Mkoani Mbeya kwa ajili ya matumizi ya kiuchumi, Mhe. Masanja amesema Serikali haioni haja ya kupunguza eneo hilo kutokana na manufaa yake kwa Taifa.

Msitu wa hifadhi wa Mbiwe, una ukubwa kilomita za mraba 491 na umeanzishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 598 la mwaka 1995.

Ahmed Ally: Tutapambana hadi kieleweke
TP Mazembe waishughulisha Young Africans