Kocha Zinedine Zidane amevunja ukimya na kueleza kuwa kuna uwezekano wa kuwakutanisha Neymar da Silva Santos Júnior anayekipiga Paris Saint-Germain (PSG), Eden Hazard anayeitumikia Chelsea na Gareth Bale katika kikosi chake cha Real Madrid.

Zidane ameyasema hayo leo alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu tetesi za usajili wa donge nono unaotarajiwa kupitia kwake, katika njia ya kuiongezea makali ya washambuliaji klabu hiyo.

Alipoulizwa kama Neymar anaweza kukamilisha ndoto yake ya kucheza katika upande mmoja na Hazard nchini Uhispania, Zidane aliwaambia waandishi wa habari, “Ndiyo. Tuna wachezaji wengi wazuri wanaotaka kuja hapa na kuichezea Real Madrid. Hiyo inawezekana lakini tuwe wavumilivu tuone kitakachotokea.”

Katika hatua nyingine, Zidane amekanusha tetesi kuwa ujio wa Hazard kwenye klabu hiyo utaiweka rehani nafasi ya Gareth Bale. Amesema tetesi kuwa wachezaji hao hawawezi kucheza pamoja ni upuuzi.

“Huo ni upuuzi, kila mchezaji mzuri duniani anaendana na mwenzake. Walisema mambo kama hayohayo kwangu mimi na [Youri] Djorkaeff, ni upuuzi tu,” aliongeza.

Santiago Bernabéu wanadaiwa kuwa kwenye wakati mgumu wa kuupata mbadala wa Cristiano Ronaldo, hali iliyozua tetesi nyingi kwa washambuliaji wengi wazuri kwa madai kuwa huenda wakaingia kwenye orodha ya mkwanja atakaokabidhiwa Zidane. Kylian Mbappé pia anatajwa kwenye orodha hiyo.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Aprili 28, 2019
Kauli ya Diamond yachochea vita kuu ya Zari na Mange, wararuana