Meneja wa klabu bingwa barani Ulaya Real Madrid, Zinedine Zidane, amesema ana matumaini kwa asilimia 150, ya kumtumia mshambuliaji Cristiano Ronaldo katika mchezo wa fainali ya ligi ya mabingwa barani Ulaya, utakaochezwa Mei 26 mjini Kiev, Ukraine dhidi ya majogoo wa jiji Liverpool.

Ronaldo ameibua mashaka ya kucheza ama kutokucheza mchezo huo, kufuatia majeraha mguu alioyapata wakati wa mchezo wa ligi ya Hispania dhidi ya FC Barcelona mwishoni juma lililopita, na kumalizika kwa sare ya kufungana mabao mawili kwa mawili.

Tayari imeshafahamika kuwa, mshambuliaji huyo kutoka nchini Ureno atakosa michezo ya ligi ya Hispania dhidi ya Sevilla siku ya Jumatano pamoja na Celta Vigo siku ya Jumamosi na mchezo wa mwisho dhidi ya Villarreal, Mei 19.

“Jambo kubwa na muhimu ni kwamba, Ronaldo ana uwezo wa kutembea pekee yake bila usaidizi wa magongo, hivyo kuna matumaini makubwa ya kupona kwa wakati na kucheza mchezo wa fainali,” amesema Zidane kuwaambia waandishi wa habari.

“Nina uhakika kila mchezaji ambaye ni majeruhi kikosini kwangu kwa sasa, atakua na uwezo wa kucheza mchezo wa fainali, ninawaambia hivyo kwa sababu nina matumaini ya asimilia 150. Kila mmoja takua katika hali nzuri kiafya Cristiano, Isco pamoja na (Dani) Carvajal.”

Real Madrid watakwenda katika mchezo wa fainali ya ligi ya mabingwa barani Ulaya wakiwa na lengo la kutwaa taji la michuano hiyo kwa mara ya tatu mfululizo, baada ya kushindwa kufanya vizuri katika michuano ya ndani ya Hispania.

Iran yamtahadharisha Trump kuhusu mkataba
Laurent Koscielny kusubiri hadi Disemba