Serikali ya Zimbabwe imepanga kuchapisha toleo jipya la noti yake yenye uwiano sawa na dola ya Marekani ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa fedha taslimu nchini humo.

Gavana wa Benki Kuu ya Zimbabwe, John Mangudya amesema kuwa noti hiyo mpya inayofahamika kama ‘bond’ itaasaidiwa na kiasi cha dola milioni 200 za Kimarekani kutoka Benki ya Africa Export-Import.

Noti hizo za dola ya Zimbabwe zitakuwa na toleo lenye thamani linganifu ya dola ya Marekani kwa mbili, tano, 10 na 20.

Kwa mujibu wa BBC, baadhi ya wateja wa mabenki mbalimbali ya Zimbabwe wameeleza kuwa wamekuwa wakikabiliwa na tatizo la kushindwa kuchukua kiasi cha dola za Marekani wanachohitaji mara kwa mara kutokana na uhaba wa fedha hizo za kigeni nchini humo.

Zimbabwe ilitangaza kuanza kutumia dola ya Marekani pamoja na fedha nyingine za kigeni baada ya kutelekeza fedha zake kutokana na mfumuko mkubwa wa bei mwaka 2009 uliolikabili taifa hilo na kupunguza kwa kiasi kikubwa thamani ya fedha yake.

 

Mahakama Kuu yamalizana na Kafulila
Bondia Amir Khan Aahidi Kutumia Mbinu Mbadala