Mbunge wa Kigoma Mjini ambaye pia ni Kiongozi Mkuu wa ACT – Wazalendo, amewajibu wanaolalamikia upangaji wa Kamati za Bunge pamoja na kile alichokiita ‘serikali kulidogosha bunge’.

Hivi karibuni, wabunge wa vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa walilalamikia uteuzi uliofanywa na Spika wa Bunge, Job Ndugai waliodai umewapanga wabunge wa upinzani wasio wazoefu kwenye kamati nyeti za kusimamia fedha ikiwemo PAC na LAAC, huku wale wazoefu wakipelekwa kwenye kamati nyingine zisizo nyeti.

Ukawa walidai kuwa uteuzi huo umefanywa kwa lengo la kuwadhibiti wabunge wa upinzani wenye nguvu.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, jana Zitto Kabwe ameandika haya:

“Kamati zote za Bunge zina hadhi sawa ndani ya Bunge. Kila mbunge ana haki ya kuwa kwenye kamati yeyote ile na hakuna mbunge bora zaidi ya mwingine. Kanuni zimeweka utaratibu wa uteuzi kwenye Kamati ikiwemo maombi ya mbunge, uzoefu na ujuzi wa eneo husika. Wanaolalamika leo upangaji wa Kamati ndio usiku wa kuamkia jana walimshinikiza Spika asiwapange mahasimu wao kisiasa kwenye Kamati wanazoona wao ni nyeti. Ni unafiki uliopitiliza unapojenga hoja ya uzoefu, chaguo la Mbunge na ujuzi wakati huo huo wenye vigezo vyote hivyo unawapiga vita kwa sababu za kisiasa. Ni dhahiri kuwa mpangilio wa Kamati unajenga Bunge kibogoyo. Nilitahadharisha toka Bunge la 11 lilipoanza kwamba, kuna dalili za Serikali kutaka kulidhibiti Bunge ( kumbukeni sarakasi za Tulia Ackson ambaye sasa ni Naibu Spika) .

Kiongozi unapokwenda kwa Spika kusema ‘fulani asipangwe Kamati fulani kwa sababu atapata sifa’ halafu ukataka ‘nyumbu’ wako ndio wapangwe huko ujue unaisadia Serikali kudogosha Bunge. Spika anapoamua Nyote, huyo usiyemtaka na nyumbu wako wasiende huko ujue amekudharau sana.

Unapoona Viongozi wa Serikali wanahangaika kupanga Kamati za Bunge watakavyo wao ujue viongozi hao ni dhaifu, hawana nia njema na hawataki kuwajibishwa.

Twendeni kwenye hizi hizi Kamati tulizopangiwa kuwafanyia kazi Watanzania. Twendeni tukaonyeshe kuwa Bunge litabaki Bunge tu na Wabunge tusikubali Bunge Kibogoyo. Ni lazima Bunge lidhibiti Serikali hata Serikali hiyo ikiwa inaongozwa na Malaika.

Serikali ni chombo cha mabavu lazima idhibitiwe, na ndio kazi ya Bunge kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 63.”

'Magufuli atauwa vyama vya upinzani nchini'
Ali Kiba aonesha Upendo kwa Diamond kwa njia hii