Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge imewahoji wabunge wa upinzani, Zitto Kabwe (ACT – Wazalendo), Halima Mdee na John Heche (Wote Chadema), kwa kufanya fujo Bungeni wakati wakipinga vikao vya bunge kutorushwa ‘Live’ na TBC.

Taarifa za kuaminika zimeeleza kuwa Mwenyekiti wa Kamati hiyo, George Mkuchika aliongoza jopo la kamati yake kumhoji Zitto kwa zaidi ya saa moja kuhusu tukio hilo lililotokea Januari 27 mwaka huu.

Kwa mujibu wa barua za mwito zilizosainiw na Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilillah, Mei 12 mwaka huu, Zitto alivunja Kanuni za Bunge kwa kusimama bila kufuata utaratibu na kuuliza jambo ambalo limeshatolewa uamuzi. Pia, aliendelea kuzungumza licha ya kuzuiwa na Spika wa Bunge.

Zitto alilitaka Bunge kuacha kujadili kwanza hotuba ya Rais na kuzungumzia uamuzi wa Serikali kutorusha ‘Live’ vikao vya Bunge, hali iliyozua mvutano Bungeni.

Mdee na Heche pia wanakumbwa na mkono wa kanuni za Bunge wakituhumiwa kwa namna walivyohusika kupinga uamuzi wa Serikali bila kufuata utaratibu.

 

Magari ya Washawasha yahamishiwa Zima Moto
Mbunge CCM anusurika kupigwa na Wabunge wa Viti Maalum Ukawa