Mshambuliaji wa Manchester United, Zlatan Ibrahimovic anajipanga kujiunga na klabu ya La Galaxy inayoshiriki Ligi kuu nchini Marekani baada ya Manchester United kukubali kuvunja mkataba wake.

Mshambuliaji huyo mkongwe ndani ya Manchester amekuwa akiandamwa na majereha ya mara kwa mara na katika mchezo wake wa mwisho kuichezea United ilikuwa disemba 2017 kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Burnley.

Bosi wa Mashetani hao wekundu, Jose Mourinho amesema mapema mwezi huu kuwa  Ibrahimovic alitaka kuondoka ndani ya timu hiyo mwishoni mwa msimu, lakini inavyoonekana safari ya kuhamia kucheza ligi kuu nchini marekani imekaribia.

“Wote tunafahamu huu ndio msimu wa mwisho kuichezea Manchester United, na itakuwa maamuzi yake binafsi kuendela kucheza au kuacha,ni majereha pekee yaliyo fanya asiendelee kuwa na msimu mzuri akiwa na sisi’’ amesema Mourinho.

Wakati huo huo, Msimu wa ligi kuu nchni Marekani (MLS) Tayari umekwishaanza huku dirisha la usajili likiwa wazi mpaka Mwezi Mei 1.

Ibrahimovic mwenye miaka 36 aliongeza mkataba wa mwaka moja kuichezea United msimu uliopita baada ya kuonesha kiwango bora katika msimu wa kwanza alipo jiunga na timu hiyo.

Aidha, Mshambuliaji huyo ambaye ameshawahi kuzichezea klabu za PSG, Barcelona, Juventus, AC Milan and Inter Milan alistaafu kuchezea timu ya taifa japo kuna taarifa huenda akarejea kutumikia taifa lake la Sweden kwenye fainali za kombe la dunia mwezi Juni,Mwaka huu nchini Urusi.

Video: DataVision International yatoa siri ya mafanikio, sasa kuikomboa jamii na vijana
Dkt Tulia: Sina uhakika kama ‘Mange’ ni binadamu wa kawaida