Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi katika Wizara hiyo amekutana na kuzungumza na Watumishi kwa ajili ya kusikiliza hoja mbalimbali pamoja na kutoa ufafanuzi wa masuala ya kiutumishi lengo likiwa ni kuhakikisha Wizara ya Nishati inazidisha ufanisi katika kuwahudumia Watanzania.

Katika kikao hicho kilichofanyika jijini Dodoma na kuwakutanisha Viongozi Wakuu wa Wizara, Menejimenti na Watumishi, Mhandisi Mramba amewakumbusha Watumishi wa Wizara kuwa Sekta ya Nishati ni nguzo muhimu katika uchumi wa nchi hivyo utendaji kazi mahiri utawezesha sekta kuchangia ukuaji wa uchumi huo.

Amesema, “tunapotekeleza majukumu yetu kila Mtumishi katika sehemu yake ya kazi anatakiwa kufanya kazi kwa weledi ili kuweza kutoa huduma bora kwa Wananchi kwa lengo la kuendeleza ukuaji wa Sekta ya Nishati.”

Akizungumzia maendeleo ya ujenzi wa jengo jipya la Ofisi za Wizara, amesisitiza kuwa jengo hilo litakuwa na Ofisi za Madereva, hivyo amewataka watumishi wa Wizara hiyo kutembelea jengo hilo ili kuona hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa mradi.

Mramba pia amewataka watumishi kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi ya viungo ili kuendelea kuimarisha afya zao kwa ajili ya kuepuka magonjwa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na magonjwa yasiyoambukizwa.

Viongozi wengine waliohudhuria kikao hicho ni Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Dkt. Khatibu Kazungu ambaye aliahidi ushirikiano ili kuhakikisha shughuli mbalimbali katika Wizara ya Nishati zinafanyika kwa lengo la kuchochea maendeleo ya Taifa.

Ushirikiano, ubunifu kuliendeleza bara la Afrika - Dkt. Tulia
Mavunde: Usimamizi Madini mkakati kukuza uchumi wa Afrika